Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 19 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 161 2017-05-08

Name

Yussuf Salim Hussein

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Chambani

Primary Question

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:-
Kumekuwa na ongezeko kubwa sana la uwekezaji katika sekta ya utalii nchini:-
Je, Serikali imejipanga vipi ili kukabiliana na ongezeko hilo?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein, Mbunge wa Chambani, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, nakubaliana na Mheshimiwa Mbunge kwamba kumekuwa na ongezeko la uwekezaji katika miundombinu na mahitaji mengine yanayochangia ukuaji wa sekta ya utalii nchini; ikiwa ni pamoja na ujenzi wa hoteli za aina na madaraja mbalimbali, uimarishaji wa vyombo vya usafiri kuelekea ndani ya hifadhi na maeneo mengine yeye vivutio na uboreshaji wa vifaa mbalimbali vinavyotumika kuhudumia watalii; mambo ambayo kwa kiwango kikubwa hutekelezwa na sekta binafsi.
Mheshimiwa Spika, kwa upande wa Serikali, pamoja na mambo mengine, ujenzi wa barabara na viwanja vya ndege uliokamilika na unaoendelea, ununuzi wa ndege mbili uliokamilika na zingine nne zinazotarajiwa kuja nchini katika siku za karibuni, zote ni jitihada zinazochangia kwa kiasi kikubwa kukua kwa sekta ya utalii nchini. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, mafanikio haya yamewezesha kuongezeka kwa idadi ya watalii ambapo mwaka 2016 idadi hiyo iliongezeka kutoka jumla ya watalii 1,137,182 wa mwaka 2015 hadi jumla ya watalii 1,284,279 kwa mwaka 2016. Hii ikiwa sawa na ongezeko la asilimia 12.9 na ongezeko linaloendelea kuonekana katika hifadhi moja kwa moja ikiwa ni pamoja na eneo la Hifadhi la Ngorongoro na Hifadhi za Taifa zinazosimamiwa na TANAPA.
Mheshimiwa Spika, ili kufanya ongezeko hilo liwe na tija na endelevu Wizara yangu imejikita katika kusimamia ubora wa huduma na utoaji huduma, kutangaza zaidi vivutio hususan vivutio vipya na kusambaza shughuli za utalii nchi nzima hususan Ukanda wa Kusini (The Southern Circuit) ili kutimiza azma ya Serikali kwa mujibu wa Mpango wa Maendeleo wa Miaka Mitano wa Mwaka 2016/2017 – 2020/ 2021 unaoainisha utanuaji wa uwigo wa mazao ya utalii (diversification of tourism products) kama mojawapo ya hatua muhimu za kuchukua (key interventions) katika kukuza utalii nchini.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatoa wito wa sekta binafsi kuongeza mbinu, bidii na mitaji kuunga mkono jitihada za Serikali katika kukuza utalii na uchumi wa Taifa kwa ujumla.