Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 19 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 159 2017-05-08

Name

Emmanuel Adamson Mwakasaka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tabora Mjini

Primary Question

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA aliuliza:-
Jimbo la Tabora Mjini hususan katika Kata za Mpera, Malolo, Mbugani na Ng’ambo (Kidongo Chekundu) kuna migogoro ya muda mrefu ya ardhi na bomoa bomoa ya nyumba za wananchi.
Je, Serikali inafanya juhudi gani kuhakikisha inamaliza migogoro hiyo ya ardhi ambayo ni kero ya muda mrefu kwa wananchi?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI ARDHI, NYUMBA, MAENDELEO NA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Emanuel Adamson Mwakasaka, Mbunge wa Tabora Mjini, kama Ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kumekuwepo na migogoro ya ardhi mingi baina ya watumiaji mbalimbali wa ardhi katika Jimbo la Tabora Mjini hususani katika kata za Mpera, Malolo, Mbugani, Ng’ambo na Kidongo Chekundu. Migogoro mingi inahusiana na madai ya fidia, kuingiliana kwa mipaka, kutozingatiwa kwa taratibu za uendelezaji, uvamizi wa maeneo yaliyopangwa kupimwa na kumilikishwa na miliki pandikizi.
Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na migogoro hiyo Serikali imekua ikichukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kufanya urasimishaji wa maeneo yote ambayo yalikuwa yamevamiwa na kujengwa kiholela ili kuweka miundombinu ya huduma muhimu katika maeneo hayo. Vilevile Serikali imeimarisha ushirikishaji wa sekta binafsi katika kuanga na kupima viwanja kwa kushirikiana na wananchi ambapo makampuni binafsi ya upangaji na upimaji yaliyosajiliwa yameshaanza kufanya kazi ya kupanga na kupima katika maeneo ya Uledi, Kariakoo na Inala. Aidha, Mpango Kabambe wa Mji wa Tabora, (Tabora Master Plan 2015 - 2035) utatoa dira ya upangaji usimamizi na uendelezaji wa ardhi katika mji wa Tabora.
Mheshimiwa Spika, Wizara yangu pia imekuwa ikisisitiza Mamlaka ya Serikali za Mitaa kuhakikisha uwepo wa fedha kwa ajili ya kulipia fidia kabla ya kufanya zoezi la uthamini wa mali kwa ajili ya utoaji wa ardhi ili kuzuia uwezekano wa kuibuka kwa migogoro ya ardhi inayohusiana na fidia. Aidha, wamiliki wa ardhi wamekuwa wakishirikiana na makampuni binafsi ya upangaji na upimaji katika hatua zote za upangaji na upimaji wa viwanja katika maeneo yao ili kuhakikisha kuwa maslahi ya pande zote yanalindwa.