Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2015-2020 | Session 7 | Sitting 19 | Youth, Disabled, Labor and Employment | Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge, Kazi, Ajira, Vijana na Walemavu | 155 | 2017-05-08 |
Name
Rhoda Edward Kunchela
Sex
Female
Party
CHADEMA
Constituent
Katavi
Primary Question
MHE. RHODA E. KUNCHELA aliuliza:-
Ipo changamoto kubwa ya ukosefu wa ajira kwa vijana wa Mkoa wa Katavi. Na hii ni kutokana na miundombinu mibovu inayosababisha wawekezaji kushindwa kuwekeza.
Je, Serikali ina mikakati gani ya kusaidia vijana hao wapate ajira na kuwa na mazingira ya kuwawezesha kujikwamua kiuchumi?
Name
Antony Peter Mavunde
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Dodoma mjini
Answer
NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU (KAZI, VIJANA NA AJIRA) alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Rhoda Edward Kunchela, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mikakati ya Serikali kusaidia vijana
wa Katavi pamoja na maeneo mengine kupata ajira na kuwa na mazingira wezeshi ya kujikwamua kiuchumi ni kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwanza ni kuzielekeza Mamlaka
za Serikali za Mitaa kuzingatia masuala ya ukuzaji ajira katika mipango ya maendeleo, hususan kutambua na kubaini mahitaji ya nguvu kazi katika maeneo husika. Kutenga na kuendeleza maeneo ya uzalishaji wa biashara kwa vijana, kuwezesha nguvu kazi kuwa na ujuzi wa kujiajiri, kuwezesha upatikanaji wa mitaji na vitendea kazi kwa makundi ya vijana, kukuza soko la bidhaa na huduma za wajasiriamali hasa vijana.
Mheshimiwa Spika, pili, kutekeleza programu ya miaka mitano ya kukuza ujuzi inayolenga kuwawezesha vijana takribani 4,419,074 kupata ujuzi wa kuajiriwa au kujiajiri katika sekta mbalimbali. Aidha, kwa mwaka wa fedha 2016/2017 vijana 1,469 wamepatiwa mafunzo ya ushonaji wa nguo kupitia viwanda vya Mazava Fabrics na Took Garment. Vijana 3,900 wametambuliwa na watapata mafunzo ya kurasimisha ujuzi wao kupitia VETA. Vijana 100 kati ya 1,001 wameanza mafunzo ya ujuzi kwa kutengeneza bidhaa za ngozi katika Chuo cha DIT, Mwanza.
Mheshimiwa Spika, tatu ni kuandaa na kuana kutekeleza Mkakati wa Kitaifa wa Kukuza Ajira kwa Vijana katika Sekta ya Kilimo (National Strategy for Youth Involvement in Agriculture) ambao unaweka mazingira wezeshi ya kuvutia vijana kujishughulisha na kilimo kwa kuwezesha upatikanaji wa ardhi, mitaji, pembejeo za kilimo, masoko, mafunzo ya ujuzi wa kilimo na ujasiriamali.
Mheshimiwa Spika, mikakati hiyo itasaidia pia kushirikisha vijana wote wa Tanzania, wakiwemo vijana wa Katavi kupata mazingira wezeshi ya kujikwamua kiuchumi. Aidha, Serikali itaendelea kuwekeza katika miundombinu ya barabara inayounganisha mikoa yote nchini ikiwemo Mkoa wa Katavi kwa lengo la kuchochea uwekezaji na kukuza fursa za ajira nchini.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved