Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 2 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 13 2016-04-20

Name

Albert Ntabaliba Obama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Buhigwe

Primary Question

MHE. DKT. HADJI H. MPONDA (K.n.y. MHE. ALBERT O. NTABALIBA) aliuliza:-
Mwaka 2011/2012 tuliweka Mkataba kati ya Halmashauri ya Buhigwe na Hospitali ya Heri Mission, Biharu Hospitali na Mulera Dispensary juu ya kutoa huduma ya matibabu kwa wazee, watoto na akinamama bure na Serikali imetoa fedha hizo na wananchi wamenufaika na huduma hizo lakini tangu Disemba, 2015 hadi sasa fedha hazitolewi tena:-
(a) Je, ni kwa nini Serikali imeacha kutoa fedha ilizokuwa ikitoa?
(b) Je, ni lini sasa fedha hizo zitaanza tena kutolewa ili huduma hizo ziendelee?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI WA TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA, UTUMISHI NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Albert Ntabaliba Obama, Mbunge wa Buhigwe lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe inatakiwa kuchangia 15% ya fedha za Mfuko wa Pamoja wa Afya katika Hospitali Teule ya Heri Mission, Kituo cha Afya Biharu na Zahanati ya Mulera. Katika bajeti ya mwaka 2015/2016, robo ya kwanza na ya pili hadi Disemba, 2015 tayari zimepelekwa shilingi milioni 27.5 katika Hospitali Teule ya Heri Mission, shilingi milioni 8.0 zimepelekwa katika Kituo cha Afya cha Biharu na shilingi milioni 8.0 zimepelekwa Zahanati ya Mulera. Fedha ambazo hazijapelekwa ni za robo tatu (Januari – Machi, 2016) na robo ya nne (Aprili – Juni, 2016) kutokana na kutopokelewa kwa fedha za Mfuko wa Pamoja wa Afya kutoka Hazina.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyoeleza katika sehemu (a) ya jibu hili, fedha ambazo hazijapelekwa katika vituo hivyo vya kutolea huduma za afya ni za robo ya tatu na robo ya nne ambazo zitapelekwa baada ya Halmashauri kupokea fedha za Mfuko wa Pamoja wa Afya (Health Busket Fund) kutoka Hazina. Napenda kutoa wito kwa Halmashauri kuimarisha usimamizi kwa kushirikiana na wamiliki binafsi wa hospitali ili makundi yanayotakiwa kutibiwa bure waweze kupata huduma hiyo.