Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 15 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 127 2017-05-02

Name

George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Primary Question

MHE. GEORGE M. LUBELEJE aliuliza:-
Kila mwaka Bunge limekuwa likipitisha Bajeti ya Serikali kuhusu Wizara, Mikoa na Wilaya lakini kumekuwa na ucheleweshwaji wa fedha zinazotengwa kwa ajili ya miradi ya maendeleo hususan katika Mikoa na Wilaya na kupelekea miradi mingi kutokamilika.
Je, ni sababu gani za msingi zinazofanya Serikali kuchelewa kuleta fedha za Miradi ya Maendeleo katika Mikoa na Wilaya?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa George Malima Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, mwenendo wa utaoji wa fedha
za utekelezaji wa Bajeti ya Serikali hutegemea mapato ya Serikali kupitia ukusanyaji wa mapato kutoka katika vyanzo vya kodi na visivyo vya kodi, mikopo pamoja na misaada kutoka kwa washirika wa maendeleo. Katika miaka ya hivi karibuni, mwenendo wa upatikanaji wa mapato ya Serikali umekuwa na changamoto nyingi katika miezi ya mwanzo wa mwaka wa fedha ambapo mikopo ya masharti ya biashara kutoka kwenye taasisi za fedha pamoja na misaada na mikopo nafuu kutoka kwa washirika wa maendeleo imekuwa haipatikani kwa wakati.
Mheshimiwa Spika, sababu kuu zinazochangia kutopatikana kwa wakati kwa fedha hizo ni pamoja na majadiliano na washirika wa maendeleo kuchukua muda mrefu, baadhi ya washirika wa maendeleo kutotimiza ahadi zao kutokana na sababu mbalimbali na kupanda kwa riba ya mikopo ya kibiashara katika soko la fedha la kimataifa.
Mheshimiwa Spika, fedha zinazokusanywa kutokana
na vyanzo vya mapato ya ndani zimekuwa zikielekezwa kugharamia matumizi mengine yasiyoepukika kama vile ulipaji wa mishahara, deni la taifa, ulipaji wa madeni ya watumishi, watoa huduma, wazabuni na wakandarasi pamoja na utekelezaji wa miradi yenye vyanzo mahususi kama vile Taasisi ya Umeme Vijijini, Mamlaka ya Elimu Tanzania, Mfuko wa Barabara, Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu, Mfuko wa Maji na Mfuko wa Reli.
Mheshimiwa Spika, sehemu kubwa ya fedha za miradi
ya maendeleo katika Sekretarieti za Mikoa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa hutumia fedha za nje. Utoaji wa fedha hizo kutoka kwa washirika wa maendeleo huzingatia mpango kazi, masharti na vigezo mbalimbali vilivyowekwa ambavyo hupaswa kuzingatiwa na mamlaka zinazotekeleza miradi.
Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kuwa miradi
ya maendeleo inatekelezwa badala ya kutegemea fedha za nje ambazo uhakika wake umekuwa hautabiriki, Serikali imeendelea kuongeza fedha za ndani kwa ajili ya kutekeleza miradi ya maendeleo hadi kufikia shilingi bilioni 8,702.7 kwa mwaka 2016/2017 ikilinganishwa na shilingi bilioni 1,366.1 mwaka 2010/2011. Aidha, Serikali yetu imeendelea kuboresha vyanzo vya ndani vya Halmashauri na kuzijengea uwezo zaidi kwa kukusanya mapato ili kutekeleza miradi mingi kwa fedha za ndani badala ya fedha za nje.