Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 15 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 123 2017-05-02

Name

Upendo Furaha Peneza

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. UPENDO F. PENEZA aliuliza:-
Tatizo la makazi duni kwa wananchi husababisha afya mbovu na hivyo kupunguza nguvu ya uzalishaji.
Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha kuwa wananchi wanapata makazi bora?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Upendo Furaha Peneza, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Ripoti ya Hali Halisi ya Miji Tanzania iliyoandaliwa na Mtandao wa Miji nchini (Tanzania Cities’ Network - TACINE) ya mwaka 2014, wastani wa kiwango cha ujenzi holela katika miji saba ya Tanzania Bara na Manispaa ya Zanzibar ilibainika kuwa ni asilimia 67 ya maneno yaliyojengeka. Mengi ya maeneo haya hayana miundombinu na huduma za msingi kama vile maji safi na salama, barabara na mifereji ya maji ya mvua na udhibiti wa maji taka na taka ngumu. Hali hiyo husababisha mafuriko, milipuko ya magonjwa, mazalio ya mbu na inzi, na mandhari mbaya ya kuishi yanayopelekea afya duni na kupunguza nguvukazi.
Mheshimiwa Spika, kutokana na hali hiyo, Serikali imeandaa programu na mikakati mbalimbali kukabiliana na hali hiyo kama ifuatavyo:-
(i) Programu ya Kitaifa ya Kurasimisha Makazi Holela Nchini ambayo inalenga mwaka 2013 mpaka 2023 inayolenga kurasimisha makazi mijini na kutoa fursa kwa maeneo kupangwa, kupimwa na kumilikishwa na kisha kutoa huduma za msingi na miundombinu.
(ii) Programu ya Kitaifa ya Kupanga, Kupima na Kumilikisha Kila Kipande cha Ardhi ya mwaka 2015 mpaka 2025 inayolenga, pamoja na mambo mengine, kuzuia kudhibiti ujenzi holela ambao husababisha kuwepo kwa makazi duni; na
(iii) Kuandaa mipango Kabambe katika Miji (Master Plans) kwa miji 30 kwa kushirikisha Halmashauri za miji na Wilaya itakayosaidia kusimamia na kudhibiti uendelezaji miji. Hadi sasa Mipango Kabambe ya Arusha, Mwanza, Singida, Tabora, Mtwara, Kibaha, Musoma, Korogwe na Songea imeandaliwa na makampuni binafsi na ipo katika hatua za mwisho za maandalizi.
Mheshimiwa Spika, natoa rai kwa mamlaka na Serikali za mitaa kutenga fedha za kutosha katika bajeti zao kila mwaka kwa ajili ya kuongeza kasi ya kupima, kupanga na kumilikisha ardhi katika maeneo yao ili kuwawezesha wananchi kupata makazi bora.