Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 1 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 8 2016-04-19

Name

Richard Phillip Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. JOHN P. KADUTU (k.n.y. MHE. RICHARD P. MBOGO) aliuliza:-
Mwaka 2009 Serikali iliwapa uraia wakimbizi toka Burundi walioingia nchini mwaka 1992 na wengine waliozaliana katika makambi ya wakimbizi ya Katumba, Mushamo na Ulyankulu:-
(a) Je, ni lini Serikali itakamilisha ahadi ya Mheshimiwa Rais ya kuwapa wakimbizi waliosalia?
(b) Ili kuondoa hali ya sintofahamu katika Sheria ya Wakimbizi Na. 20 inayokataza mikusanyiko zaidi ya watu watano, je, ni lini Serikali itafuta hadhi ya makambi ya wakimbizi katika maeneo ya Katumba?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Richard Philip Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Mbunge, napenda kurekebisha swali hilo kwamba ni kweli mwaka 2009 Serikali iliwapa uraia wakimbizi toka Burundi walioingia nchini mwaka 1972 na siyo mwaka 1992. Pia hakuna Sheria ya Wakimbizi Na. 20 bali ipo Sheria ya Wakimbizi Na. 9 ya mwaka 1998. Vilevile maeneo aliyoyataja Mheshimiwa Mbunge ni makazi ya wakimbizi na siyo makambi ya wakimbizi na hakuna mkimbizi aliyepo kambini aliyepewa uraia.
Mheshimiwa Spika, Serikali kwa kushirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la kushughulikia Wakimbizi (UNHCR) ipo katika hatua za mwisho kufanya uhakiki kamili kwa wakimbizi walengwa ili kutoa uraia kwa wanaostahili, kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi. Tunategemea hadi kufikia mwisho wa mwaka huu kazi hii itakuwa imekamilika ili taratibu za kutoa uraia kwa mujibu wa sheria ziweze kufanyika.
Mheshimiwa Spika, Kifungu cha 20 cha Sheria ya Wakimbizi Na. 9 ya mwaka 1998 kinahusu wakimbizi na hasa kililengwa kwa wakimbizi waliopo makambini katika makazi ya Katumba, Ulyankulu na Mishamo. Wengi wa wakazi wake sasa ni raia, sio wakimbizi. Kwa hiyo, kifungu hicho hakiwahusu kwa kuwa sasa wakazi wengi wa Katumba, Ulyankulu na Mishamo wameshapewa uraia. Wizara yangu kwa kushirikiana na TAMISEMI inaandaa utaratibu wa kufuta utengefu wa maeneo haya ili viwe vijiji vya kawaida kwa mujibu wa sheria.