Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 9 2016-01-26

Name

Marwa Ryoba Chacha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. MARWA R. CHACHA aliuliza:-

Mheshimiwa Spika, kumekuwepo na uvamizi wa tembo kutoka Hifadhi ya Serengeti na kupelekea vifo na uharibu wa mashamba katika Wilaya ya Serengeti na maeneo jirani:-

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kunusuru maisha na mali za Watanzania waishio Serengeti?

(b) Je, Serikali ina mpango wa kutathimini upya fidia inayotolewa kwani haiendani na uhalisia wa uharibifu wa mali na upotevu wa maisha ya watu?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa spika, kwa kuwa hii ni mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako Tukufu katika jukumu hili nililopewa, napenda nimshukuru Mwenyezi Mungu na kwa kweli namrudishia sifa na utukufu. Lakini pia napenda kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa uteuzi huu na kwa kweli natoa ahadi kwamba sitomwangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, Mbunge wa Serengeti lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, kutokana na madhara yanayosababishwa na wanyamapori hususani Tembo, Serikali imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ili kunusuru maisha na mali za wananchi waishio kando ya Hifadhi ya Taifa ya Serengeti. Hatua hizo ni pamoja na zifuatazo:-

i. Kuunda timu ya udhibiti wa wanayamapori hatari na waharibifu ambayo inajumuisha watumishi kutoka kikosi dhidi ya ujangili cha Bunda, Hifadhi ya Taifa ya Serengeti, Pori la Akiba Ikorongo, Halmashauri ya Wilaya na Mwekezaji Grumeti Reserves. Lengo ni kuhakikisha kwamba tukio lolote la uvamizi wa tembo linashugulikiwa kwa haraka iwezekanavyo.

ii. Kuweka minara au madungu (observation towers) ambayo hutumiwa na Askari Wanyamapori katika kufuatilia mwenendo wa tembo ili wanapotaka kutoka nje ya maeneo ya hifadhi hatua za kuwadhibiti zichukuliwe mapema, kama ilivyofanyika katika Kijiji cha Rwamchanga mpakani na Pori la Akiba la Ikorongo.

iii. Kutumia teknolojia ya mizinga ya nyuki ambayo huwekwa pembenzoni mwa mashamba na kufanya tembo wanapoingia katika mashamba yenye mizinga kufukuzwa na nyuki.

iv. Kutoa elimu ya uhifadhi kwa jamii ili wananchi waepuke kulima kwenye shoroba za wanyamapori pamoja na umuhimu wa kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi.

Mheshimiwa Mwenyeikiti, aidha, Serikali ina mpango unaoendelea wa kutumia ndege zisizokuwa na rubani (UAV) kwa ajili ya kufukuza tembo. Mafunzo kuhusu matumizi ya ndege hizo yanaendelea kutolewa kwa watumishi kwa kushirikiana na Taasisi ya World Animal Protection (WAP).

(b) Mheshimiwa Spika, kulingana na Kifungu cha 71 cha Sheria ya Uhifadhi Wanyamapori Na. 5 ya mwaka 2009, Waziri mwenye dhamana ya Maliasili amepewa mamlaka kuandaa kanuni za malipo ya kifuta jasho au machozi kwa wahanga wa wanyamapori hatari. Aidha, Kanuni ya 3 ya Kanuni za malipo ya kifuta jasho au machozi za mwaka 2011, inaainisha kuwa malipo hayo yatafanyika endapo mwananchi atajeruhiwa au kuuawa, ama kuharibiwa mazao au mifugo na wananyamapori. Malipo hayo huzingatia uwezo wa fedha na upatikanaji wa taarifa za kweli kutoka kwa wahanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, Wizara itaendelea kurejea kanuni na viwango kadri hali ya maisha inavyobadilika.