Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 1 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 05 2017-04-04

Name

Ignas Aloyce Malocha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Primary Question

MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:-
Serikali ilituthibitishia kuwa gesi aina ya Helium iligundulika katika Ziwa Rukwa na kwamba gesi hiyo ina thamani kubwa na ni adimu sana duniani:-
Je, ni lini sasa Serikali itaanza kuchimba gesi hiyo ili Watanzania waanze kunufaika na gesi hiyo kabla haijagunduliwa au kuchimbwa mahali pengine duniani?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, Mbunge wa Kwela, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba kampuni ya Helium One Limited imefanya utafiti wa gesi ya Helium katika Bonde la Ziwa Rukwa. Taarifa za awali zinaonesha uwezekano wa kuwepo kwa gesi ya Helium kiasi cha futi za ujazo bilioni 54 katika maeneo ya Ziwa Rukwa. Matokeo haya yanatokana na uchunguzi wa sampuli tano za mavujia ya gesi ya Helium katika maeneo hayo, kiasi ambacho kinakadiriwa kuwa kikubwa zaidi ya mara sita ya mahitaji ya dunia kwa sasa.
Mheshimiwa Spika, Kampuni ya Helium One Limited imefanya utafiti huo kupitia kampuni zake tanzu za Gogota (TZ) Limited, Njozi (TZ) Limited na Stahamili (TZ) Limited zinazomiliki leseni za utafutaji wa gesi ya Helium katika Ziwa Rukwa. Kampuni hizi zilipewa leseni za utafutaji wa Helium katika maeneo mbalimbali kuanzia mwaka 2015. Shughuli za utafutaji wa kina wa gesi ya Helium unaendelea kwa kukusanya taarifa zaidi za kijiolojia, kijiokemia, kijiofizikia na 2D ili zitumike kwa ajili ya uchorongaji wa visima vya utafiti wa gesi asilia kilichopo katika maeneo hayo.
Mheshimiwa Spika, uchimbaji wa gesi ya Helium utaanza mara baada ya kazi ya utafiti wa kina, upembuzi yakinifu na tathimini ya athari za mazingira kukamilika. Baada ya utaratibu kukamilika, uchorongaji katika maeneo ya Ziwa Rukwa unatarajiwa kuanza mwaka 2018.