Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 9 Energy and Minerals Wizara ya Madini 115 2016-02-05

Name

Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. OSCAR R. MUKASA aliuliza:-
Mgodi wa Stamigold, Biharamulo uko kijijini Mavota katika Wilaya ya Biharamulo na wananchi wa Kijiji cha Mavota kwa sasa hawana fursa hata kidogo ya kufanya uchimbaji mdogo mdogo licha ya kwamba mgodi huo upo kijijini kwao, hali ambayo imekuwa chanzo kikubwa cha migogoro inayosababisha uvunjifu wa amani:-
(a) Je, Serikali iko tayari kuwa na mazungumzo ya kimkakati na wananchi wa Kijiji cha Mavota kupitia Mbuge wao kwa manufaa ya uwekezaji na wanakijiji wa Mavota?
(b) Kama Serikali haiko tayari kufanya mazungumzo hayo, je, ni kwa sababu zipi?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimwa Oscar Rwegasira Mukasa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ipo tayari kuwa na mazungumzo na wananchi wa Kijiji cha Mavota kwa lengo la kuwawezesha wananchi hao kutumia fursa zilizopo katika Mgodi wa Stamigold karibu na Mavota. Mgodi huo kwa sasa unamilikiwa na Serikali kwa asilimia 100 kupitia STAMICO ambapo Stamigold kampuni tanzu ya STAMICO ndiyo inayofanya shughuli za uchimbaji.
Mheshimiwa Naibu Spika, mambo muhimu yatakayozingatiwa ni pamoja na kutenga maeneo kwa ajili ya wachimbaji hao wadogo, kuwaelimisha namna ya kupata mitaji ya uchimbaji ikiwa ni pamoja na kutumia fursa za kuomba ruzuku Serikalini. Kadhalika, pamoja na kuwapa elimu na kuwahamasisha kuunda vikundi vya uchimbaji ili waweze kusaidiwa kwa pamoja. Aidha, Mgodi wa Biharamulo utawapatia mafunzo ya utaalamu wa kuchimba madini pamoja na kuwafundisha kanuni za usalama, afya na utunzaji wa mazingira katika migodi yao. Lakini pia watapewa mafunzo kwa vitendo katika mgodi wa Stamigold pale itakapohitajika kufanya hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, mgodi huo uko tayari na ulishaanza kuwasaidia wananchi wa Kijiji cha Mavota. Kati ya tarehe 26 na 30 Juni, 2015, Mavota Gold Mine Group kilipewa ushauri wa namna bora ya kuendesha shughuli za uchimbaji na utafiti wa dhahabu katika eneo walilomilikishwa leseni. Kikundi hicho kilimilikishwa leseni ya uchimbaji mdogo yenye Namba PL 001493WLZ iliyotolewa tarehe 23 Februari, 2015. Eneo hilo lina ukubwa wa hekta 9.43.
Mheshimiwa Naibu Spika, mgodi umetoa fursa za ajira kwa vijiji vya jirani. Vijana wenye ajira za muda mrefu kutoka vijiji vya jirani ni 15 na wafanyakazi wenye mikataba ya muda mfupi ni 54.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mgodi umetoa fursa za kibiashara kwa vikundi vitatu kutoka vijiji vya Mavota pamoja na Mkukwa ambapo wanavikundi hushirikiana kutafuta mazao ya kuuza mgodini kwa kuwasilisha mazao hayo kila wiki. Mazao hayo ni pamoja na viazi vitamu, mihogo, mboga za majani pamoja na matunda. Kutokana na kufanya biashara na Stamigold kati ya kipindi cha Julai 2014 na Disemba 2015, vikundi vyote vitatu vimeweza kujipatia zaidi ya shilingi milioni 200.