Bunge la Tanzania
Jamhuri ya Muungano ya Tanzania
Term | Session | Sitting | Sector | Ministry | Qn No | Date |
---|---|---|---|---|---|---|
2015-2020 | Session 6 | Sitting 4 | Industries and Trade | Viwanda na Biashara | 51 | 2017-02-03 |
Name
Eng. Atashasta Justus Nditiye
Sex
Male
Party
CCM
Constituent
Muhambwe
Primary Question
MHE. ENG.ATASHASTA J.NDITIYE aliuliza:-
Nchi yetu bado ina upungufu mkubwa sana wa sukari na kwa kuwa Wilayani Kibondo kuna ardhi oevu kwenye Bonde la Mto Malagarasi na Lupungu ipatayo ekari 52,000 na wananchi wako tayari kutoa ushirikiano kwa matumizi ya ardhi hiyo.
Je, Serikali haioni umuhimu wa kutafuta mwekezaji wa kiwanda cha sukari katika eneo hilo?
Name
Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji
Sex
Female
Party
CCM
Constituent
Kondoa
Answer
NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO (K.n.y WAZIRI WA VIWANDA, BIASHARA NA UWEKEZAJI) alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Viwanda, Biashara na Uwekezaji, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Atashasta Justus Nditiye, Mbunge wa Muhambwe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa kuwa katika Nchi yetu kuna upungufu wa sukari kama alivyoeleza Mheshimiwa Mbunge. Viwanda vyetu vyote kwa pamoja vina uwezo wa kuzalisha tani 300,000 za sukari ya mezani na hakuna uzalishaji wa sukari ya viwandani ilihali mahitahi ya Sukari kwa matumizi ya nyumbani na viwandani ikikadiriwa kuwa tani 610,000 hivyo uhitaji wa uwekezaji katika sekta hiyo ya viwanda vya sukari ni mkubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuondoa upungufu huo, Serikali imeshatambua na inaendelea kuainisha maeneo yanayofaa kwa kilimo cha miwa na uzalishaji wa sukari katika Mikoa mbalimbali ikiwemo Morogoro, Mara, Pwani, Songwe na Kigoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Bonde la Mto Malagarasi lililopita katika vijiji kumi vya Kasaya, Kibuye, Kigina, Kukinama, Kumsenga, Kumshwabure, Magarama, Nyakasanda, Nyalulanga na Nyarugusu ni moja ya maeneo ambayo Serikali imeyaainisha kwa ajili ya kilimo cha miwa na uzalishaji wa sukari. Tayari Halmashauri ya Wilaya ya Kibondo kwa kushirikiana na Wananchi na Kampuni ya Green Field Plantations imefanya vikao vya uhamasishaji katika vijiji vyote kumi na hivi karibuni wataanza taratibu za upimaji wa ardhi. Mradi huu utahusisha jumla ya hekta 25,000 sawa na ekari 61,776 ambapo Kampuni ya Green Field Plantations italima hekta 20,000 na itawasaidia wakulima wadogo pembejeo na teknolojia ili waweze kulima hekta 5,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho nimshukuru Mheshimiwa Mbunge na Mkuu wa Wilaya ya Kibongo kwani barua walizotuma Wizarani ziliongeza kasi hii, tuendelee kushirikiana.
Copyright © Bunge Polis 2021. All Rights Reserved