Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 3 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 40 2017-02-03

Name

Oliver Daniel Semuguruka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza:-
Mkoa wa Kagera umezungukwa na nchi za Rwanda, Burundi na Uganda na mipaka ya nchi hizo imekuwa adhabu kwa wananchi wa Mkoa wa Kagera, kwani hali ya usalama wa raia na mali zao umekuwa mashakani kutokana na kuvamiwa na majambazi toka nje ya Tanzania wakishirikiana na baadhi ya Watanzania wasio na uzalendo na Taifa lao.
Je, Serikali ina mikakati gani ya kuimarisha ulinzi katika mipaka hiyo ili wananchi wa Mkoa wa Kagera waweze kuishi kwa amani na utulivu?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli yako matukio ya ujambazi katika mikoa ya pembezoni ikiwemo Kagera ambapo watu toka nchi jirani wanaingia na silaha kali za kivita na kufanya unyang‟anyi wa mali za wananchi. Hii inatoka na mkoa huu kupakana na nchi ambazo zimekosa amani na kuzalisha wahamiaji haramu kuingia nchini kwetu kwa njia za panya na tukizingatia kwamba mipaka yetu imezungukwa na mapori makubwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia vyombo vya ulinzi na usalama inafanya mikakati ya kutekeleza yafuatayo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, vyombo vya ulinzi na usalama vinafanya operesheni za pamoja katika mipaka yetu; vyombo vya ulinzi na usalama vya nchi yetu na nchi ya jirani vinafanya operasheni za pamoja na kubadilishana taarifa mbalimbali za uhalifu na wahalifu.
Mheshimiwa Naibu Spika, vyombo vya ulinzi na usalama hufanya misako ya kushitukiza katika mapori yote yaliyoko Kagera, Kigoma na maeneo yote ya mipakani, kwani ndiyo maficho ya uhalifu; hufanya doria na polisi kusindikiza magari katika baadhi ya maeneo tete; Kamati za Ulinzi na Usalama za maeneo husika zinafanya vikao vya ujirani mwema ili kuwaelimisha wananchi juu ya kutoa taarifa kwenye Mamlaka za Serikali husika wanapoona wageni wasiofahamika wanaingia ama kutoka katika maeneo yao.