Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 1 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 3 2017-01-31

Name

Ester Alexander Mahawe

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTER A. MAHAWE aliuliza:-
Wilaya ya Simanjiro haina Hospitali ya Wilaya na hivyo kusababisha mateso kwa wakazi wa maeneo mbalimbali ya Wilaya hiyo hususan wanawake ambao wanakosa huduma za kujifungua lakini pia kutokana na uchache wa vituo vya afya na zahanati.
(a) Je, ni lini Serikali itavipa hadhi vituo vya afya vya Mererani na Orkesment ili kupunguza tatizo?
(b) Wilaya ya Simanjiro ina gari moja tu la wagonjwa; je, ni lini Serikali itapeleka gari lingine kwenye Kituo cha Afya Mererani ili kuokoa maisha ya akina mama wajawazito?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA Alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ester Alexander Mahawe, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Manyara lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Spika, maombi ya kupandisha hadhi Kituo cha Afya Orkesment kinachomilikiwa na Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) kuwa Hospitali Teule ya Wilaya tayari yamewasilishwa katika Wiazara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto mwezi Oktoba, 2016 kwa uamuzi, baada ya kujadiliwa na kukubalika katika vikao ngazi ya Halmashauri na Mkoa. Kibali kikipatikana Serikali itaingia mkataba rasmi wa utoaji huduma na mmiliki wa kituo hicho ili kuainisha majukumu ya kila mdau. Aidha, Halmashauri imepokea shilingi milioni 80.0 zilizotengwa katika bajeti ya mwaka 2016/2017 kwa ajili ya ujenzi wa wodi ya wazazi katika kituo cha afya cha Urban Orkesment kinachomilikiwa na Serikali. Taratibu za kumpa Mkandarasi zinaendelea.
(b) Mheshimiwa Spika, Halmashauri imetenga gari moja ambalo linatumika kutoa huduma za dharura kwa wagonjwa wenye rufaa. Gari hilo hutoa huduma kwa wagonjwa katika vituo vyote kikiwemo Mererani pale inapotokea dharura.
Hata hivyo, gari hilo ni chakavu kiasi cha kuhitaji matengenezo ya mara kwa mara. Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro imeshauriwa kuweka kipaumbele na kutenga bajeti katika mwaka 2017/2018 kwa ajili ya ununuzi wa gari la kuhudumia wagonjwa.