Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 3 Youth, Disabled, Labor and Employment Maswali kwa Waziri Mkuu 32 2016-11-03

Name

Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Primary Question

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA aliuliza:-
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli akiwa Mwanza alipiga marufuku na kuziagiza mamlaka zinazohusika kuacha kuwasumbua wafanyabiashara wadogo wadogo maarufu kama Wamachinga:-
Je, Serikali inatekeleza agizo hilo kwa kiwango gani?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, (TAMISEMI), naomba kujibu swali la Mheshimiwa Maftaha Abdallah Nachuma, Mbunge wa Mtwara Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, mantiki ya agizo la Mheshimiwa Rais akiwa Mwanza ilikuwa ni kutowahamisha wafanyabiashara wadogo katika maeneo walipo endapo hakuna maeneo mbadala yaliyotengwa kwa ajili ya biashara zao. Mikoa na Halmashauri zimeendelea kutimiza malengo ya kuweka mazingira mazuri kwa wafanyabiashara wadogo kwa kutenga maeneo rasmi ya kufanyia biashara na kuboresha yaliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, maeneo yaliyotengwa rasmi kwa wafanyabiashara wadogo katika Halmashauri ya Manispaa ya Mtwara ni Likonde, Mbae na Mjimwema. Vilevile, Halmashauri inaboresha Soko la Skoya ambalo halitumiki kwa muda mrefu kutokana na kujaa maji wakati wa mvua. Kazi zinazofanyika ni kurekebisha mitaro ya kupitisha maji ili eneo hilo liweze kutumika kama ilivyokusudiwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kutumia fursa hii kuzikumbusha Halmashauri zote nchini kutenga maeneo kwa ajili ya wafanyabiashara wadogo kutokana na umuhimu wao katika kukuza kipato na ajira. Aidha, wafanyabiashara wadogo wanatakiwa kuzingatia sheria na kuhakikisha wanaendesha biashara katika maeneo yaliyotengwa rasmi ili kuepuka usumbufu.