Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 7 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 95 2016-09-15

Name

Stephen Hillary Ngonyani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Primary Question

MHE. STEPHEN H. NGONYANI aliuliza:-
Shamba la Mkonge la Hale Mwakinyumbi lilimilikiwa na Chavda Ltd. lakini Serikali ililitoa shamba hilo kwa wananchi wa Hale kwa matumizi yao lakini hulimwa huku wakiwa na wasiwasi kila wakati.
Je, kwa nini Serikali isiwakabidhi rasmi wananchi wa Hale shamba hilo ili wawe na utulivu wanapoendelea na shughuli zao za kilimo?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali namba 95 la Mheshimiwa Stephen Hillary Ngonyani, Mbunge wa Korogwe Vijijini kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, Shamba la Mwakinyumbi ni shamba linalomilikiwa na Kampuni ya Mwakinyumbi Sisal Estates Ltd. ya M/s Chavda. Bwana Chavda alinunua shamba hili kwa Mamlaka ya Mkonge Tanzania wakati wa awamu ya kwanza ya ubinafsishaji wa mashamba ya mkonge mwaka 1985 na 1988.
Mheshimiwa Spika, wakati wa ubinafsishaji sehemu ya shamba hili lilitolewa kwa wananchi wa vijiji vya Mwakinyumbi Stesheni na Hale kwa ajili ya makazi na kilimo cha mazao ya chakula. Shamba hili limeacha kuzalisha tangu mwaka 1994 baada ya kutelekezwa na mmiliki.
Mheshimiwa Spika, mnamo tarehe 20 Julai, 2016 nilifanya ziara Mkoani Tanga na katika ziara hiyo nilitembelea mashamba ya Mwakinyumbi, Magunga, Magoma na Kwashemshi yaliyopo katika Wilaya ya Korogwe. Katika kulikagua shamba la Mwakinyumbi, tulibaini kuwa shamba hili limevamiwa na wananchi na taasisi mbalimbali kwa shughuli za kilimo na uchimbaji kokoto.
Mheshimiwa Spika, tayari Wizara yangu ilishatoa maelekezo kwa Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe kuanza utaratibu wa ubatilisho wa miliki hiyo. Hata hivyo, katika kutekeleza maelekezo haya mnamo tarehe 5 Agosti Halmashauri ilituma ilani ya siku 90 ya kusudio la kufuta miliki ya shamba hilo.
Mheshimiwa Spika, ili wananchi wa Korogwe waweze kukabidhiwa sehemu ya shamba hilo rasmi kupitia Halmashauri yao, taratibu za ubatilisho lazima zikamilishwe. Ninatoa rai kwa wananchi wa Korogwe kuwa na subira wakati Serikali inashughulikia suala hili.
Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge lako Tukufu, nitoe rai pia kwa Halmashauri zote nchini kuendelea kuainisha mashamba pori na viwanja vilivyotelekezwa ili mchakato wa kisheria wa kufuta milki zake ufanyike kwa wakati na kuondoa migogoro inayozidi kushamiri siku hadi siku.