Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 7 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 94 2016-09-15

Name

Daniel Nicodemus Nsanzugwako

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Primary Question

MHE. ENG. ATASHASTA J. NDITILE (K.n.y MHE. DANIEL N. NSANZUGWANKO) aliuliza:-
Miji mingi nchini inakabiliwa sana na uhaba wa Maafisa Ardhi na Maafisa Mipango Miji.
(a) Je, ni kwa nini Serikali isianzishe utaratibu wa kuajiri Maafisa hawa moja kwa moja wanapohitimu Vyuo Vikuu?
(b) Je, ni kwa nini Serikali isichukue jukumu la kununua vifaa vya kupimia ardhi kama vile darubini, GPS na kadhalika na kuvisambaza kwenye Miji yetu ikiwemo Mji wa Kasulu?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Nicodemus Nsanzugwanko, Mbunge wa Kasulu Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kuna upungufu mkubwa wa wataalam katika sekta ya ardhi na tafiti zinaonesha kwamba hadi kufikia Machi, 2016 idadi ya wataalam wa sekta ya ardhi kwa maana ya Maafisa Ardhi, Mipango Miji na Wapima Ardhi, Wathamini na Mafundi Sanifu katika Halmashauri 161 ilikuwa ni 1,087 ukilinganisha na mahitaji ya wataalam 3,040. Idadi hii ni sawa na asilimia 36 ya mahitaji kamili ya watumishi hao. Tafsiri ya mapungufu haya imekuwa ikionekana katika kiwango kidogo cha upangaji, upimaji na umilikishwaji wa ardhi iliyopimwa mijini na vijijini.
(a) Mheshimiwa Spika, kuhusu utaratibu wa kuajiri maafisa moja kwa moja wanapohitimu Vyuo Vikuu, Serikali imekuwa ikichukua jitihada mbalimbali ili kukabiliana na tatizo hilo. Mathalani katika kipindi cha mwaka huu wa fedha 2016/2017 Wizara yangu imeomba kibali cha kuajiri watumishi wapya 252 katika sekta ya ardhi. Kama kibali hicho cha kuajiri kitapatikana basi nina uhakika pengo litapungua ingawa ni kwa kiasi kidogo.
Hata hivyo nimshukuru Mheshimiwa Mbunge kwa kuliona hili na nimwahidi kuwa Serikali imechukua wazo lake na pia itaendelea kulifanyia kazi.
(b) Mheshimiwa Spika, kuhusu ununuzi wa vifaa vya upimaji, Wizara yangu tayari imetenga kiasi cha shilingi bilioni nane katika bajeti ya mwaka 2016/2017 kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji ambavyo vitasambazwa katika ofisi zetu za Kanda na hata hivyo Halmashauri za Wilaya, Miji na Majiji ndizo zenye dhamana ya kusimamia upimaji wa ardhi kwenye maeneo yao, hivyo zinapaswa kutenga fedha kwa ajili ya kununua vifaa vya upimaji. Aidha, katika kukabiliana na upungufu wa vifaa vya upimaji, Wizara imekuwa ikinunua vifaa vya kupimia ardhi na kuvisambaza kwenye Halmashauri kila fedha zinapopatikana.