Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 38 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 314 2016-06-07

Name

Japhet Ngailonga Hasunga (CPA)

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Vwawa

Primary Question

MHE. JAPHET N. HASUNGA aliuliza:-
Kuwepo kwa Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya nchini kumekuwa kukileta migongano katika utekelezaji wa sera na shughuli mbalimbali za maendeleo nchini:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuupitia upya mfumo wa ugatuaji wa madaraka (D by D) ili kuweza kuuboresha na kupunguza migongano mbalimbali ya kiutendaji?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Japhet Ngailonga Hasunga, Mbunge wa Vwawa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wakuu wa Mikoa wapo kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 katika Ibara ya 61(1) mpaka (5) na majukumu yake yamefafanuliwa vizuri katika Ibara ya 61(4) kwamba atakuwa na wajibu wa kusimamia utekelezaji wa kazi na shughuli zote za Serikali katika eneo lake.
Mheshimiwa Naibu Spika, dhana ya Ugatuaji wa Madaraka kwa Umma (Decentralization by Devolution) pia inatokana na Ibara ya 145 na 146. Madhumuni yake ni kupeleka madaraka kwa wananchi yakiwemo madaraka ya kisiasa, kifedha, kiutawala ili kusogeza huduma karibu na wananchi. Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya ni wasimamizi wa sera, sheria, kanuni na miongozo katika Mikoa na Wilaya wanayoongoza.
Mheshimiwa Naibu Spika, Viongozi hao kisheria hawaruhusiwi kuingilia (interference) maamuzi na utendaji wa Serikali za Mitaa endapo hakuna sheria au taratibu zilizokiukwa kimaamuzi. Hata hivyo, wamepewa mamlaka na sheria kuingilia kati (interventions) endapo maamuzi yatakayofanywa na Serikali za Mitaa yatakiuka sera, sheria na miongozo iliyopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, mahusiano kati ya Serikali Kuu na Serikali za Mitaa yamebadilika kutoka kwenye dhana ya utoaji amri na upokeaji amri au mdhibiti na mdhibitiwa, kuwa ya mashauriano, majadiliano na maelewano. Vilevile, Ofisi ya Rais, TAMISEMI imeendelea kufanya vikao vya pamoja na Wizara za Kisekta ili kuwa na uelewa wa pamoja wa dhana ya ugatuaji na mantiki yake katika kusogeza karibu huduma kwa wananchi.