Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 40 Energy and Minerals Wizara ya Madini 343 2016-06-10

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Primary Question

MHE. VICKY P. KAMATA (K.n.y MHE. CONSTATINE J. KANYASU) aliuliza:-
Mgodi wa GGM - Geita umepewa eneo la ukubwa wa kilometa za mraba 192 kwa ajili ya kuchimba dhahabu wakati wananchi wamenyang‘anywa maeneo yao.
Je, ni lini maeneo waliyonyang‘anywa wananchi yatarudishwa kwa wananchi?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini napenda kujibu swali la Mheshimiwa Constatine John Kanyasu, Mbunge wa Geita Mjini lililoulizwa kwa niaba yake na Mheshimiwa Vicky Kamata Likwelile, Mbunge wa Geita Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Kampuni ya Geita Gold Mine Limited yaani GGM inamiliki leseni ya uchimbaji mkubwa wa madini kupitia leseni namba SML45/99 yenye ukubwa wa kilometa za mraba 196.27 iliyopewa kwa mujibu wa Sheria ya Madini.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maeneo ambayo mgodi GGM waliyahitaji ndani ya leseni yao kwa ajili ya uchimbaji walifanya mazungumzo na wamiliki wa maeneo hayo na kulipa fidia kwa mujibu wa Sheria Namba Nne ya Madini ya 2010 pamoja na Sheria Namba Tano ya Ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanaomiliki ardhi ndani ya leseni ya GGM kwa ajili ya makazi na shughuli mbalimbali ambazo siyo shughuli za uchimbaji wanaendelea na shuhguli zao kama kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo baadhi ya wamiliki wa leseni za uchimbaji mdogo ambao hawakufikia makubaliano na mgodi wa GGM bado wanamiliki leseni zao za uchimbaji mdogo. Baadhi ya wananchi hao ni pamoja na Bwana Jumanne Mtafuni mwenye leseni ya uchimbaji mdogo PML0001044 pamoja na Bwana Leonard John Chipaka mwenye leseni namba PML0001331 wachimbaji wadogo hawa wanaendelea na shughuli za uchimbaji katika maeneo yao kama kawaida.
Mheshimiwa Naibu Spika, kulingana na maelezo haya sasa wananchi ambao wamepisha maeneo baadhi yao walilipwa fidia kwa mujibu wa taratibu za nchi hii.