Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 7 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 83 2016-02-03

Name

Mwantum Dau Haji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MWANTUMU DAU HAJI aliuliza:-
Kwa kuwa barabara kuu kwenda mikoani zina foleni na tukiangalia barabara hizo zinatumika na magari mengi ya mizigo ambayo mara nyingi huwa ni chanzo cha ajali na Watanzania wengi kupoteza maisha:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha ajali hizo zinapungua?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Mwantumu Dau Haji, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyowahi kujibiwa swali la msingi namba 13, 74, 75 na 167, katika Mikutano mbalimbali ya Bunge la Kumi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, zipo sababu nyingi za vyanzo vya ajali za barabarani nchini. Utafiti wa kisayansi unaonesha kuwa, sababu hizo zimegawanyika katika makundi makuu matatu:-
Kwanza, sababu za kibinadamu kama vile ulevi na uzembe zinazochangia asilimia 76 ya ajali zote.
Pili, ubovu wa vyombo vya usafiri zikiwemo hitilafu za kiufundi na mfumo wa umeme wa magari unaochangia asilimia 16.
Tatu, mazingira ya barabara yaani ubovu, ufinyu na usanifu mbaya wa barabara zetu unachangia asilimia saba tu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni dhahiri kuwa, suala la msongamano wa magari ambao linahusiana zaidi na mazingira ya barabara linachangia kiasi kidogo cha ajali ikilinganishwa na sababu zingine nilizozitaja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la ajali nchini ni tatizo ambalo kutokana na madhara yake kwa umma, Serikali itaendelea kukabiliana nalo kwa nguvu zote. Kwa kuzingatia hali hii, Jeshi la Polisi, Kikosi cha Usalama Barabarani likishirikiana na wadau wengine wa usalama barabarani limechukua hatua zifuatazo:-
(1) Kusimamia kwa karibu mifumo ya sheria ukiwemo utaratibu mpya wa malipo ya papo kwa papo (notification) kwa njia ya kielektroniki ulioanzishwa hivi karibuni katika Jiji la Dar es Salaam na baadaye kutumika kwa nchi nzima.
(2) Kunyang‟anya leseni za madereva wazembe wanaorudia kutenda makosa ya usalama barabarani ikiwa ni pamoja na kuwakamata na kuwafikisha Mahakamani pindi wanaposababisha ajali.
(3) Kuwafukuza au kuwabadilisha kazi Askari wa Usalama Barabarani wanaotuhumiwa kujihusisha katika vitendo vya rushwa ambavyo vimekuwa vikichochea ongezeko la ajali barabarani.
(4) Kutoa elimu na namba za simu za viongozi wa Kikosi cha Usalama Barabarani kwa wananchi ili wafahamu haki zao wanapokuwa abiria au watumiaji wa barabara na kutoa taarifa wanapotendewa isivyo halali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitumie fursa hii kupitia Bunge lako Tukufu kuwaagiza madereva na watumiaji wengine wa barabara kote nchini kuzingatia Sheria za Usalama Barabarani na kutoa taarifa za dereva, askari au mtu yoyote anayekiuka sheria za barabarani au taratibu za kazi kwa makusudi ili hatua stahiki zichukuliwe.