Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 40 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 336 2016-06-03

Name

George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Primary Question

MHE. GEORGE M. LUBELEJE aliuliza:-
Serikali ilikwishaanza kujenga vituo vya afya katika vijiji vya Mima na Mbori na ujenzi huo umesimama kutokana na ukosefu wa fedha.
Je, Serikali ina mpango gani wa kukamilisha ujenzi wa vituo hivyo ili wananchi wa maeneo hayo wapate huduma za afya?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Malima Lubeleje, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa jengo la Kituo cha Afya Mima ulianza mwaka 2008/2009 ambapo mpaka sasa umegharimu kiasi cha shilingi milioni 60. Jengo la wagonjwa wa nje (OPD) liko katika hatua ya umaliziaji. Kazi ambazo hazijakamilika ni uwekaji wa dari, samani pamoja na vifaa tiba. Ili kumaliza kazi hiyo zimetengwa shilingi milioni 15 katika bajeti ya mwaka 2016/2017. Aidha, imejengwa nyumba ya watumishi ambayo imekamilika kwa gharama ya shilingi milioni 48.
Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa ujenzi wa jengo la Kituo cha Afya Mbori ulianza katika mwaka wa fedha 2011/2012 ambapo mpaka sasa umegharimu kiasi cha shilingi milioni 82. Kazi zilizofanyika ni upauaji, upakaji rangi nje na ndani, uwekaji wa madirisha ya vioo pamoja na kupiga dari. Kazi zilizobaki ni pamoja na ufungaji wa umeme, ufungaji wa milango ya ndani 16, ufungaji wa taa na uwekaji wa mfumo wa maji safi na taka. Katika mwaka wa fedha 2015/2016, kituo hiki kilitengewa shilingi milioni 15 ili kumalizia kazi zilizobaki na shilingi milioni 35 zimetengwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 ili kujenga nyumba ya watumishi (two in one).