Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 40 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 334 2016-06-10

Name

Martha Jachi Umbulla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARTHA J. UMBULLA aliuliza:-
Kamati za Fedha za Mipango za Halmashauri za Wilaya ni Kamati muhimu sana kwa Wabunge wote kushiriki bila kujali ni wa Viti Maalum au wa Jimbo kwa sababu zinashughulika na masuala ya fedha, bajeti na mipango ya miradi ya maendeleo; na kwa muda mrefu sasa Wabunge wa Viti Maalum wamekuwa wakiomba kuondolewa kwa sheria kandamizi na ya kibaguzi ya kuwazuia kushiriki katika Kamati hizo:-
(a) Je, Serikali iko tayari kusikiliza kilio cha Wabunge wa Viti Maalum ili kuwaruhusu kushiriki kwenye Kamati hizo?
(b) Je, Serikali iko tayari kufuta sheria hiyo kandamizi na yenye ubaguzi ambayo haina tija na hasa ikizingatiwa kuwa ilitungwa mwaka 1998 wakati ambao Ubunge wa Viti Maalum bado haujaanza?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Wajumbe wa Kamati za Kudumu za Halmashauri wametajwa katika kifungu cha 75(6) cha Sheria, Sura 287 ya Mamlaka za Serikali za Wilaya na kifungu cha 47(4) cha Sheria Sura 288 ya Mamlaka za Miji. Kwa mujibu wa sheria hizo mbili, Wajumbe wa Kamati hawatazidi theluthi moja (1/3) ya Madiwani wote isipokuwa Kamati ya Fedha na Mipango ambayo Wajumbe wake ni wale wanaoingia kwa nyadhifa zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, upatikanaji wa Wajumbe wa Kamati ya Fedha na Mipango umefafanuliwa katika Kanuni za Kudumu za Uendeshaji wa kila Halmashauri ambapo Wajumbe wake ni Mwenyekiti au Meya wa Halmashauri ambaye atakuwa Mwenyekiti, Makamu Mwenyekiti au Naibu Meya wa Halmashauri, Mbunge au Wabunge wa Majimbo wanaowakilisha majimbo katika eneo la Halmashauri, Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Halmashauri na Wajumbe wengine wasiozidi wawili watakaopendekezwa na Mwenyekiti/Meya kisha kupigiwa kura na Baraza la Halmashauri mmoja kati yao awe mwanaume au mwanamke. Hivyo, ili Wabunge wa Viti Maalum waweze kushiriki kwenye Kamati za Fedha tutahitaji kubadili sheria kwanza ili pendekezo hilo liweze kutekelezeka.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kama ilivyoelezwa katika sehemu (a) ya jibu hili, Wajumbe wa Kamati ya Fedha na Mipango wataendelea kuwa ni wale waliotajwa katika Sheria na Kanuni za Mamlaka za Serikali za Mitaa hadi hapo sheria itakapofanyiwa marekebisho kwa kushirikisha wadau mbalimbali.