Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 49 2016-09-09

Name

Hassan Elias Masala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nachingwea

Primary Question

MHE. HASSAN E. MASALA aliuliza:-
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwamilikisha na kutoa Hati za Kimila kwa wananchi wa Nachingwea?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hassan Elias Masala, Mbunge wa Nachingwea, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Nachingwea ina jumla ya vijiji 127, hadi kufikia mwaka 2007 vijiji 104 vilikuwa tayari vimefanyiwa upimaji. Kati ya hivyo 104, vijiji 99 tu ndiyo vilikuwa vimepata vyeti vya vijiji na hapo vijiji 22 ndiyo vilikuwa vimewekewa mpango wa matumizi bora ya ardhi. Mwaka 2009 Vijiji vya Mbondo, Nakalilonji na Nahimba vilikuwa katika mchakato wa kuandaliwa Hati Miliki za Kimila pamoja na ujenzi wa Masijala ya Ardhi kwa ufadhili wa MKURABITA ambao haukukamilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa kukamilisha wananchi na kutoa Hati za Haki Miliki za Kimila ni sehemu ya utekelezaji wa Sheria ya Ardhi Na. 5 ya mwaka 1999 na Kanuni zake. Hati na Haki Miliki za Kimila siyo tu zinawahakikishia wananchi usalama wa miliki zao bali pia huwawezesha wananchi kuzitumia kama dhamana za mikopo pale wanapohitaji kukidhi vigezo vya mikopo.
Mheshimiwa Naibu Spika, juhudi zinazofanywa na Halmashauri mpaka sasa ni kutenga fedha katika bajeti zao ili kukamilisha zoezi la utoaji wa hati 1,170 ambazo hazikukamilishwa na MKURABITA. Aidha, Halmashauri imejiwekea mkakati wa kutayarisha hati nyingine 1,170 na kuzigawa kwa wananchi wa Vijiji vya Mbondo, Nakalonji, Nahimba na Namatunu ifikapo 2017. Jukumu la Halmashauri za Wilaya ni kutenga fedha katika bajeti zao ili kuwezesha utoaji wa hati za haki miliki za kimila kwa kufuata sheria, kanuni na miongozo inayotolewa na Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaipongeza Ofisi ya Mbunge wa Nachingwea kwa kuwezesha pia kufanikisha zoezi la uandaaji wa Hati Miliki za kimila katika Kijiji cha Namatunu kwa kutumia fedha za Mfuko wa Jimbo ambapo mpaka sasa jumla ya hati 66 zimeandaliwa. Nitoe rai kwa Wakurugenzi wa Halmashauri kuendelea kutenga fedha katika bajeti zao ili wananchi wote wenye uhitaji katika Halmashauri zetu waweze kupata haki ya kumiliki ardhi zao ili kuinua pia vipato vyao.