Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 42 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 360 2016-06-14

Name

Hamadi Salim Maalim

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kojani

Primary Question

MHE. HAFIDH ALI TAHIR (K.n.y. MHE. HAMADI SALIM MAALIM) aliuliza:-
Jeshi la Polisi ni chombo muhimu kinacholinda usalama wa raia na mali zao. Askari hawa wanapomaliza mafunzo yao kwa ngazi mbalimbali kama vile Sajenti, Staff Sajenti, Meja na nyingine, hucheleweshwa sana kulipwa maslahi yanayoendana na vyeo vyao:-
Je, ni kwa nini Askari hao hawalipwi kwa wakati?

Name

William Tate Olenasha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ngorongoro

Answer

NAIBU WAZIRI WA KILIMO, MIFUGO NA UVUVI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Hamadi Salim Maalim, Mbunge wa Kojani, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Askari Polisi hupanda vyeo kama ilivyo kwa watumishi wengine wa umma na vyeo hivyo huambatana na kuongezeka kwa maslahi yao kulingana na cheo kilichopandishwa. Mwaka 2014/2015 jumla ya Askari 1,657 wa vyeo vya uongozi mdogo walipandishwa vyeo mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kumekuwepo na ucheleweshaji wa ulipwaji wa mishahara inayolingana na vyeo katika Jeshi la Polisi. Serikali mara zote imekuwa ikijitahidi kurekebisha mishahara ya vyeo vipya kwa haraka iwezekanavyo kwa Askari waliopanda vyeo. Yapo matatizo ya kiufundi yaliyojikeza wakati wa zoezi la kurekebisha mishahara na kutokea baadhi ya Askari kutorekebishiwa mishahara yao. Hata hivyo, juhudi hufanyika ili kutatua tatizo hilo mara mhusika anapowasilisha malalamiko yake Polisi Makao Makuu. Kitengo cha Maslahi Makao Makuu hupokea malalamiko na kuwasiliana na mamlaka za ulipaji ili kutatua tatizo hili. Aidha, naomba nitoe wito kwa Askari yeyote ambaye amepatwa na tatizo hili awasiliane na viongozi katika Kamandi yake au Makao Makuu ya Polisi, Idara ya Maslahi ili kupata ufumbuzi wa tatizo hili haraka iwezekananvyo.