Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 42 Energy and Minerals Wizara ya Madini 359 2016-06-14

Name

Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Primary Question

MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-
Katika Wilaya ya Tunduru iko miradi mingi ya REA ambayo kampuni mbili zimepewa kazi hiyo lakini wakandarasi wanasuasua kukamilisha miradi hiyo na muda wake umeisha kwa kigezo cha kutolipwa:-
Je, ni lini Serikali itatoa pesa kukamilisha miradi hiyo?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Iddi Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatekeleza mradi kabambe wa REA Awamu ya II katika Wilaya ya Tunduru na kazi hii imeshaanza na inatarajiwa kukamilika mwishoni mwa mwezi huu, mwaka 2016. Kazi ya kupeleka umeme katika Wilaya ya Tunduru inaunganisha pia kazi ya ujenzi wa njia ya umeme Msongo wa kilovoti 33 yenye urefu wa kilometa 293.2, ujenzi wa njia ya umeme Msongo wa kilovoti 0.4 yenye urefu wa kilometa 77.1 lakini pia ufungaji wa transfoma 38 zenye ukubwa mbalimbali.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kazi hizo, kazi nyingine inayofanyika ni kuwaunganishia umeme wateja wa awali 3,330 lakini pia mradi umekamilika kwa asilimia 79 ambapo ujenzi wa laini kubwa umekamilika kwa asilimia 83, laini ndogo asilimia 74, transfoma saba zimeshafungwa na wateja 182 wameshaunganishiwa umeme. Gharama ya mradi wa Mkoa wa Ruvuma ikiwemo Wilaya ya Tunduru ni shilingi bilioni 32.56. Kiasi ambacho mkandarasi hadi sasa ameshalipwa ni shilingi bilioni 27.22 ambayo ni sawa na asilimia 83.6. REA wanasubiri kupata uthibitisho kutoka kwa mkandarasi kuhusu madai ya shilingi bilioni 3.19 ili aweze kulipwa mara tu baada ya uthibitisho huo.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Tunduru vijiji vinne vya Jimbo la Tunduru Kusini ambavyo ni Azimio, Chiwana, Mbesa na Mkandu, vimeunganishiwa miundombinu ya umeme ambayo inafanyiwa marekebisho na matayarisho kwa ajili ya kuwashwa. Hivi sasa mkandarasi anaendelea kufunga transfoma na mita za Luku katika vijiji vingine 34 ambavyo vimesalia katika Wilaya ya Tunduru ili viweze kupatiwa umeme ifikapo tarehe 30 Juni, 2016.