Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 22 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2017-05-11

Name

Jaku Hashim Ayoub

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Primary Question

MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa umakini na utendaji wake na kilichonivutia zaidi anapotoka hapa akienda ofisini kwake haifiki hata dakika, watu anaokutana nao njiani anasalimiana nao ni jambo la kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri bila kujali itikadi ya chama. Ninakupongeza sana, mara nyingi huwa nikikaa nje pale na nikienda kunywa chai ninakuona. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu tunakaribiwa na Mwezi Mtukufu wa Ramadhani kama wiki mbili tu panapo majaaliwa tukifika, hali ya kusikitisha ya Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, sukari inahitajika kwa wingi matumizi yake. Hata wananchi wa Ruangwa na Peramiho wanahitaji sukari. Mwenyezi Mungu alitupa mtihani wa mvua, viwanda vyetu vya ndani havikuweza kuzalisha sukari ya kutosha na uchunguzi au harufu niliyoipata tunahitaji kama tani laki moja na ushee. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kusikitisha kwa taarifa niliyo nayo ni kuwa mmetoa vibali vya tani 30,000 na baya zaidi kuna msemo Waislamu husema nguo ya Ijumaa hufuliwa Alhamisi na mvua hii pengine isikauke. Sasa hawa mliowapa vibali, sukari yao navyotegemea hata ikifika Ramadhani itakwisha, itawasaidia nini wananchi? Mnatumia utaratibu gani kuwapa vibali hawa watu, wanarudia ndiyo wale wale au na wengine? Kuna formula gani ili kuokoa hatua hii.

Mheshimiwa Waziri Mkuu uko tayari kuleta watu angalau mwezi huu Mtukufu wa Ramadhani wakaingiza sukari kwa kipindi hiki ili kuokoa hii hali na janga hili lilivyo? Hii sukari mliyowapa vibali hata ikifika Ramadhani itakwisha, itasaidia nini kwa wananchi?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaku, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, najua amezungumza mengi na yaliyotengeneza maswali mengi sana. jambo la msingi alilotaka kuzungumza hapa ni kupungua kwa sukari na mahitaji ya sukari nchini kwa sasa. Napenda niwathibitishie Watanzania kwamba Serikali iko macho na inajua maeneo gani yanahitaji kuboreshwa kulingana na mahitaji ambayo yanahitajika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa suala la sukari ni kweli nchi yetu hatuna uzalishaji wa kutosha wa sukari kutosheleza mahitaji ya Watanzania. Katika mwaka wa kilimo, mahitaji ya sukari nchini ni zaidi ya tani 420,000, lakini uzalishaji tulionao hapa nchini ni tani 320,000; kwa hiyo tunakuwa na mapungufu ya sukari inayohitajika ya tani laki moja na ikiwezekana zaidi kwa sababu ya ongezeko la watumiaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kila mwaka tunao utaratibu wa kuagiza sukari na mwaka huu pia tumesahafanya hilo, tumeshaagiza sukari na mwaka huu tumeagiza sukari tunataka tuagize sukari ya tani 131,000 kwa mujibu wa takwimu zilizofanyiwa utafiti na Bodi ya Sukari, kati ya hizo tayari tumeshaagiza tani 80, kati ya tani 80 tayari zimeshaingia tani 35 na nyingine ziko bandarini. Hizi tani 35 tumeshaanza kuzigawa kwenye maeneo yote ya nchi ili ziweze kufika kwa wananchi ziweze kusaidia kupunguza gharama na bei.

Mheshimwa Naibu Spika, pia kwa kuwa, tunakabiliwa na Mwezi Mtukufu wa Ramadhani ambapo watumiaji ni wengi, utaratibu wa kuagiza sukari zaidi kufikia malengo umeshaandaliwa. Watanzania tushirikiane kuwasihi wafanyabiashara ambao sasa hivi wamepandisha bei bila sababu na hii inaumiza sana Watanzania kwa sababu bei zilizopandishwa hazina umuhimu wowote kwa sababu uzalishaji tulionao na hii sukari pengo tunavyoleta nchini inataka tu bei zile ziendelee kuwa ambazo zinaweza kuhimilika na Watanzania wenzetu.

Mheshimiwa Naibu Spika, iko mikakati ya kuongeza uzalishaji kufikia malengo. Natambua tuna viwanda vinne, Kagera Sugar, Kilombero, TPC na Mtibwa, tuna kiwanda cha tano kilichoko Tanzania Visiwani, Mahonda navyo pia vinasaidia uzalishaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuondoa tatizo la kuagiza sukari nje ya nchi, tumejiwekea utaratibu wa kukutana na wafanyabiashara wenye viwanda na kuwasihi kuongeza uzalishaji na tumeona jitihada kadhaa ambazo zinafanywa na wazalishaji. Bahati nzuri sana wiki moja iliyopita nilikuwa Mkoani Kilimanjaro, nimepata nafasi ya kutembelea kiwanda cha TPC ambacho kimeonesha mafanikio makubwa ya uzalishaji zaidi. Mwaka jana walizalisha tani 100,000 na sasa wameongeza tani 20,000, kwa hiyo, sasa hivi wamefikia uwezo wa kuzalisha tani 120,000 na msimu huu wa kilimo wataongeza tani nyingi zaidi, hivyo hivyo na viwanda vingine kama Kilombero na Mtibwa Sugar.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nilipofanya ziara Mkoani Manyara, nilitembelea Manyara Sugar, kwa hiyo viwanda vingi vinaendelea kujengwa na sasa tunakamilisha taratibu za kuanza ujenzi wa kiwanda cha sukari Mkoani Morogoro kuna eneo la Mbigiri kwa ushirikiano na Magereza pia na eneo la Mkulazi ambalo linaandaliwa na Taasisi ya NSSF na PPF kwa pamoja na wawekezaji ambao pia wako tayari kutuunga mkono katika uzalishaji wa sukari. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaondoe mashaka Watanzania kwamba sukari ipo na wakati wa Ramadhani sukari ya kutosha itakuwepo wala hakuna sababu ya kuongeza bei, tutafanya hivyo na pia ufuatiliaji kuona bei haziongezeki ili kuwakera Watanzania.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister