Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 10 Public Service Management Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2017-04-20

Name

Venance Methusalah Mwamoto

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kilolo

Primary Question

MHE. VENANCE M. MWAMOTO: Mheshimiwa Spika, nami naomba nimuulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kwa kuwa moja ya sababu ambazo zilipelekea wananchi wengi kutoa ridhaa kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi kuongoza ilikuwa ni ahadi nzuri ambazo zilitolewa. Pamoja na kuwa ahadi hizo nyingi zimeanza kutekelezwa lakini kulikuwa kuna kilio kikubwa sana cha wafanyakazi kwa ujumla kutokana na malimbikizo ya madeni na mishahara yao na hasa walimu. Serikali inasemaje kuhusu suala hili ili waweze kupata moyo wa kuona kweli zile ahadi ambazo walipewa na mgombea wa Chama cha Mapinduzi zimetekelezwa?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Venance Mwamoto Mbunge wa Kilolo kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali tunao watumishi wengi walimu wakiwemo na kama watumishi kwa sababu wanafanya kazi zao za kila siku na nyingine zinahitaji kulipwa malipo ya ziada mbali na malipo ya mshahara, nikiri kwamba tunadaiwa na watumishi wetu ikiwemo na walimu pia. Hata hivyo, Serikali yetu imeahidi kumaliza kwa kiasi kikubwa kero hii ya madeni kutoka kwa watumishi wetu wa Serikali walimu wakiwemo. Hatua ya awali ambayo tumeichukua ni kufanya mapitio ya madeni yetu yote tunayodaiwa na watumishi ikiwemo na walimu.
Mheshimiwa Spika, madeni ya walimu yote yalishakusanywa na yalihakikiwa kwanza na Wakaguzi wa Ndani wa kila Halmashauri mahali walipo lakini madeni yale pia yameendelea kuhakikiwa na Mkaguzi Mkuu wa Serikali kwa maana ya timu ambayo imeundwa pamoja na Wizara ya Fedha ili kuona uhalali wa madeni hayo baada ya kuwa tumegundua kuwa baadhi ya madeni yamepandishwa kwa kiasi kikubwa ambayo sio halali. Kwa hiyo, kila hatua tunayoifikia ya kukusanya madeni na kuyahakiki tukishapata kiwango tunaendelea kulipa. Kwa hiyo, Serikali imeendelea kulipa madeni ya wafanyakazi na inataka iwahakikishie wafanyakazi kwamba madeni yao yatalipwa na hiyo ndiyo stahili yao na kwa sababu tumeanza kulipa, tunaendelea kulipa kadri ambavyo tunamaliza kuhakiki ili tuweze kuondokana na madeni haya. Pia Serikali haijaishia hapo. Tumeweka utaratibu wa kudhibiti uzalishaji wa madeni kwa watumishi wetu na kusisitiza watu wafuate Kanuni na taratibu za eneo linazozalisha madeni ili tuweze kuondoa madeni ambayo sio muhimu wakati mwingine. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini nataka nitumie nafasi hii pia kusema kwamba baadhi ya madeni ambayo hayana viwango vikubwa yanaweza kulipwa kwenye Halmashauri zenyewe mbali ya kulipwa na Serikali Kuu. Lazima nimshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa Jiji la Arusha ambaye kupitia mapato yake ya ndani na kupitia Baraza lake la Madiwani waliweza kulipa madeni ya watumishi wao hasa walimu ya zaidi ya shilingi milioni mia moja na zaidi. Kwa hiyo, mfano huu ni mzuri kwa Wakurugenzi wengine kwenye Halmashauri nyingine ili kuondoa kero kwenye maeneo yao. Wanaweza kutenga fedha kupitia mapato yao ya ndani kulipa watumishi wao wakiwemo walimu ili kuondokana na ule mlolongo ambao tunatakiwa tuuhakiki. Wakishahakiki wakijiridhisha na hasa baada ya kuwa tumedhibiti madeni na wao wanaweza kuruhusu kazi fulani zifanywe, wazitengenezee bajeti ili waweze kulipa moja kwa moja kuondokana na kero zinazoweza kupatikana kwa wafanyakazi.

Additional Question(s) to Prime Minister