Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 10 Industries and Trade Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2017-04-20

Name

Godbless Jonathan Lema

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Arusha Mjini

Primary Question

MHE: GODBLESS J. LEMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru na mimi kunipa nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.
Mheshimiwa Spika, tunafahamu jitihada za Serikali ya Awamu hii ya kupigania sera ya Tanzania ya viwanda ambalo ni jambo muhimu sana kila mtu mwenye akili timamu analipongeza. Hata hivyo, ili suala la viwanda liweze kuwa ni la uhakika na kweli ni lazima investors ama wafanyabiashara wawe na mazingira huru na mazingira yasiyokuwa na mashaka katika utekelezaji wa shughuli zao za kila siku za biashara ili kuelekea katika investment hizo za viwanda.
Mheshimiwa Spika, Tanzania Revenue Authority (TRA) wamekuwa wakitesa na kusumbua sana wafanyabiashara hasa wa mikoa mikubwa kama Dar es Salaam, Arusha, Mwanza na Mbeya. Katika kila mkoa na hasa mimi nakotoka Arusha, TRA wamekuwa wakitumia Polisi, Usalama wa Taifa na TAKUKURU kuwasumbua wafanyabiashara, kuwatishia mpaka kesi za money laundering kwenye masuala yanayohusu kodi. Sasa ili wafanyabiashara hawa waweze kufanya kazi zao kwa uhakika na waweze kuwa na confidence ya uwekezaji katika Taifa hili, nini kauli ya Serikali juu ya mfumo wa TRA unaotumika sasa wa kusumbua na kuwapa taabu wafanyabiashara katika shughuli zao za kila siku?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Godbless Lema, Mbunge wa Arusha kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, ni ukweli kwamba tunacho chombo ambacho kinawajibika katika ukusanyaji wa kodi kutoka kwa walipa kodi wetu wakiwemo wafanyabiashara. Pia wafanyabiashara hawa pamoja na haki yao ya kulipa ambayo kila mmoja ni wajibu wake kulipa tunatambua kwamba wako wafanyabiashara ambao wana madeni sugu. Jambo ambalo nalieleza nimelishuhudia pia hata kwenye televisheni na tuliwahi kupata taarifa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha pale ambapo TRA kupitia chombo chake Makao Makuu kiliunda task force ya ufuatiliaji wa madeni sugu kwa wadaiwa sugu na wadaiwa sugu wale si wote lakini wachache hawataki kabisa kulipa pamoja na kwamba wanajua wao ni wadaiwa sugu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, task force ilikuwa na mkakati wa kuwapitia wadaiwa sugu wale wachache ili waweze kulipa madeni yao. Sasa ile task force iliundwa kwa pamoja na TRA wenyewe, kulikuwa na Jeshi la Polisi pamoja na TAKUKURU ili kuona kuwa wanapokwenda kule hakutumiki vitendo ambavyo havikubaliki kama vile utoaji wa rushwa ili madeni hayo yasilipwe au namna nyingine yoyote ambayo pia mfanyabiashara anaweza kuona kwamba si sahihi kwake. Kwenye msafara ule tuchukue mfano wa Arusha tulipata taarifa kwamba Polisi walikuwa wanatembea na silaha lakini si kwa lengo la kumtisha mfanyabiashara ni kwa sababu ya utaratibu ambao jeshi inao hasa wanapokwenda kufuata fedha kama zinaweza kulipwa papo kwa papo. Kwa hiyo, ile ilileta mtikisiko kidogo kwa wafanyabiashara.
Mheshimiwa Spika, nataka nitumie nafasi hii pia kumshukuru Mkuu wa Mkoa wa Arusha kwamba aliita wafanyabiashara pamoja na TRA na kueleza kwanza umuhimu wa ulipaji kodi kila mmoja atambue na walipaji sugu watambue kwamba ni haki yao kulipa kodi kwa biashara ambayo wameifanya. Pia alieleza vyombo vyetu zile silaha iwe ni kwa ajili ya kulinda tu ule msafara kwa sababu pia wanahusika kukusanya fedha lakini sio kwa ajili ya kumtisha mfanyabishara. Kwa hiyo, aliweza kurudisha amani na kuondoa mashaka waliyonayo wafanyabiashara na kuwafanya wafanyabiashara na TRA kuwa marafiki na huo ndio msisitizo wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, lakini nataka niwaambie wafanyabiashara kwamba TRA inao utaratibu wa wafanyabiashara ambao wanadhani wanatendewa sivyo. TRA imeunda dawati ambalo liko katika kila mkoa la kusikiliza kero za wafanyabiashara pindi inapotokea kuna vitendo ambayo si sahihi. Kwa hiyo, watumie madawati hayo kupeleka malalamiko yao na tunaamini madawati hayo yatafanya vizuri. Jambo la msingi kwa wafanyabiashara na walipa kodi wote ni kufahamu kwamba ni muhimu kulipa kodi kwa ajili ya maendeleo yetu.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie kwamba Serikali inaheshimu wafanyabiashara, Serikali inatambua wawekezaji wote pamoja na wale wanaoendesha viwanda na maeneo mengine na tutawapa ushirikiano, waendelee kutambua umuhimu wao wa kulipa kodi na sisi tutaheshimu kodi yao wanayotupa na kila mmoja ajue wajibu wake. TRA yetu kama ambavyo tumesema iendelee kutoa elimu kwa wafanyabiashara na walipa kodi wote ili tuweze kupata kodi kwa njia ambayo haimpelekei hofu mfanyabiashara. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Godbless Jonathan Lema

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Arusha Mjini

Question 1

MHE. GODBLESS J. LEMA: Mheshimiwa Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa majibu yake. Kwa sababu TRA ina sheria zake na kwa sababu amekiri kwamba hii task force inakuwa-engaged kwa wale wafanyabiashara ambao ni wadeni sugu wa TRA. Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa vile kuna sheria zinazoendesha shirika hili la kodi, ni kwa nini sheria hizo zisitekelezwe kwa kina na kwa uthabiti kuliko kutumia task force ya Jeshi la Polisi, TAKUKURU pamoja na Usalama wa Taifa kitu ambacho kinatia hofu sana wafanyabiashara hao.
Mheshimiwa Spika, ukweli ni kwamba TAKUKURU, Usalama wa Taifa na Jeshi la Polisi hawafahamu mambo yanayohusu kodi. Sasa hata kama ni task force kwa nini isiwe inahusisha TRA wenyewe pamoja na sheria zao za kodi ambazo zinajulikana nini kitafanyika iwapo mfanyabiashara ataendelea kukaidi kulipa kodi katika Taifa hili?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mheshimiwa Godbless Lema kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimesema task force ni kwa ajili ya wale ambao kwa makusudi hawataki kutekeleza sheria ya ulipaji wa kodi kwa kuwatembelea kwenye maeneo yao, siyo wote ni wachache wale sugu. Nimeeleza kwamba task force hii imejengwa na TRA wenyewe Polisi na TAKUKURU na hapa kila mmoja ana wajibu wake. Kama mlipa kodi anaamua kulipa mpaka afuatwe na kwa sababu wanakusanya fedha Polisi yeye yuko pale kwa ajili ya ulinzi wa fedha ambayo inakusanywa. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, TAKUKURU yuko pale kuona kwamba hakuna nafasi ya rushwa kutokea. Kwa sababu pale inakwenda kumuuliza na wakati mwingine mlipa kodi sugu anaweza kudhani kwamba anadaiwa fedha nyingi akatamani kufanya makubaliano na Afisa wa TRA kwa lengo la kutoa rushwa. Kwa hiyo, mtu wa TAKUKURU yuko pale kuhakikisha kwamba hakuna jambo lolote linalohusiana na rushwa linalofanywa kati ya mdaiwa sugu ambaye hakutaka kulipa yeye mwenyewe labda angeweza kushawishi alipe kidogo ili jambo lake liweze kuisha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kila mmoja ana wajibu wake lakini mwenye dhamana kubwa pale ni TRA kukumbushia sheria, kuonyesha kipindi ambacho amekaa bila kulipa na kwamba sasa anatakiwa kulipa kodi na kwa kuwa ni mdaiwa sugu basi pale inaonekana kwamba hataki kuchukua hatua hiyo wanatakiwa kumpeleka Polisi hata kama itakuwa alikuwa hana notisi. Kwa hiyo, timu ile inalenga zaidi kuhakikisha kwamba hakuna vitendo vya uovu vinavyoendelea kwenye uendeshaji wa zoezi lile lakini halilengi kumtisha mfanyabiashara. Polisi hawajibiki kumtisha wala TAKUKURU hausiki na mfanyabishara isipokuwa ni TRA mwenyewe kama ambavyo nimeeleza.
Mheshimiwa Spika, kwa hili nataka niwahakikishie wafanyabiashara, pamoja na haya yote yanayoendelea kwamba task force inapita kwenye maeneo haya haina nia mbaya kabisa na wafanyabiashara wetu na wawe na amani. Cha msingi zaidi kila mmoja sasa aone umuhimu wa kulipa kodi bila shuruti ili shughuli zetu ziweze kwenda kama ambavyo tumekubaliana.