Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 3 Livestock , Fisheries, Agriculture, Food Security and Cooperatives Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2017-02-02

Name

Kiswaga Boniventura Destery

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Magu

Primary Question

MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa mujibu wa taratibu za kisera tulizonazo, Serikali ina wajibu wa kuangalia hali ya chakula nchini. Kwa taarifa ya Serikali, Halmashauri 55 zina upungufu wa chakula. Je, Serikali ina mpango gani wa haraka wa kuleta chakula ili kupunguza mfumuko wa bei ulioko sokoni sasa?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Magu, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la chakula limeelezwa vizuri sana na Waziri wa Kilimo kupitia taarifa Bungeni juzi na taarifa yake imefafanua vizuri na hatua ambazo Serikali inazichukua za kuhakikisha kwamba Watanzania wanaendelea kuwa na akiba ya kutosha kwenye maeneo yao ili Watanzania waweze kuwa na uwezo wa kuendelea na uzalishaji mwingine.
Mheshimiwa Naibu Spika, sikusudii kurudia maelezo ya Mheshimiwa Waziri, lakini Serikali inaendelea kuwahamasisha wafanyabiashara wa ndani pia kutumia nafasi hii kufanya biashara kutoka Wilaya moja ambayo ni kwenye mazao mengi kwenda maeneo mengine ili kuweza kuongeza idadi ya chakula na kupunguza bei kwenye masoko na tunao ushahidi wa kutosha kwamba Mikoa ya Rukwa, Mbeya Songwe, Njombe, Iringa, Ruvuma bado ina chakula cha ziada, lakini pia hata kwenye soko letu la Kimataifa - Kibaigwa kuna mahindi ya kutosha.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, wafanyabiashara wa ndani watumie nafasi hiyo kuweza kuchukua chakula na kupeleka kwenye maeneo ambayo yana upungufu. Hata jana tulikuwa tunazungumza pia na Mheshimiwa Mathayo, Mbunge wa Same Mashariki namna ambavyo Same imekuwa kame wakati wote, hata msimu ambao tunakuwa na mvua nyingi, kuona namna nzuri ambayo tunaweza kuwasaidia kupata chakula kwa kutumia pia hata wafanyabiashara wa ndani zaidi ya majibu ya Mheshimiwa Naibu Waziri.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia tumeanza kushuhudia kuona mvua zikinyesha ingawa siyo nyingi za kutosha, lakini basi pale ambako tunapata mvua angalau mara moja, mara mbili, tunawahamasisha wakulima kulima mazao ya muda mfupi ili yaweze kuiva kwa kipindi kifupi pia tuweze kujipatia chakula kwa msimu ujao wa chakula.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama kutakuwa na tatizo lolote lile, Serikali hii iko bado inajua na inafuatilia mwenendo wa hali ya chakula na ufumbuzi tutaupata kupitia Serikali yenyewe.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Kiswaga Boniventura Destery

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Magu

Question 1

MHE. KISWAGA B. DESTERY: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kumshukuru sana Waziri Mkuu kwa ufafanuzi mzuri na ambao kweli ulitolewa na Waziri wa chakula. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sababu tunayo makundi mawili, kundi ambalo lina uwezo wa kifedha lakini bei iko juu na utaratibu wa Serikali ni kuwapelekea ili kwenda kupunguza mfumuko wa bei, lakini tunalo kundi pia ambalo lilitajwa na Waziri wa Kilimo, kaya kama 3,000 hivi ambazo zina hali mbaya na hazina uwezo hata wa kununua chakula. Je, Serikali sasa ina mpango gani wa kuhakikisha kwamba jambo hili linaenda kuwasidia wananchi wake?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, suala la uwezo mkubwa, mdogo au wa kati wa kifedha ni jambo pana ambalo kila mmoja na katika kila familia inayo utaratibu wa kujiongezea uchumi kwenye maeneo yao badala ya Serikali kuwaahidi kwamba tutawapelekea fedha ili kuwaongezea fedha; na kwa kuwa tumesema chakula sasa kinapanda kwenye masoko, ni kweli, lakini ni kwa sababu ya hofu ya hali ya hewa ambayo tunayo ya msimu huu wa kilimo, watu wengi wameweka chakula ndani wakidhani, kutumia nafasi hiyo wanaweza kujipatia fedha nyingi. Jambo hili halikubaliki kimsingi kwa sababu tunawaumiza wale ambao wana kipato cha chini kwa ujumla wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata kama hali ya chakula inakuwa nzuri, bado tuna kundi la watu ambao hawana uwezo wa kifedha. Muhimu zaidi watanzania wote tutambue umuhimu wa kila mmoja kuwa lazima apate chakula, aweze kupata mavazi, aweze kupata malazi kwa kile kidogo alichonacho.
Kwa hiyo, wafanyabiashara wetu nawasihi sana, tusijenge tabia ya kupandisha bei vyakula au bidhaa zetu bila sababu yoyote ile ili iweze kuwawezesha wale wote ambao wamezoea kuishi katika maisha ya kawaida, maisha ya kati na wale wapate chakula, waweze kupata huduma nyingine ili pia waweze kuendesha maisha yao. Huo ndiyo msingi imara wa jambo hilo.