Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 6 Sitting 3 Justice and Constitutional Affairs Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2017-02-02

Name

Freeman Aikaeli Mbowe

Gender

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Hai

Primary Question

MHE. FREEMAN A. MBOWE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kuniona lakini nilisikitika kwamba unadai hujaniona, lakini nashukuru umeniona hatimaye. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue fursa hii kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali la msingi la kisera.
Mheshimiwa Naibu Spika, leo ni siku ambayo Taifa letu linaadhimisha siku ya Haki Duniani. Tunapoadhimisha siku hii ya Haki Duniani ambayo nina hakika leo Spika wetu yupo Dar es Salaam kwa ajili ya jukumu hilo akiungana na viongozi wengine wa Kitaifa akiwemo Mheshimiwa Rais na Jaji Mkuu. Ni miezi mitatu kamili tangu Mheshimiwa Godbless Lema, Mbunge wa Arusha akamatwe nje ya geti la Bunge na kupelekwa kizuizini kushtakiwa kwa kesi inayoitwa ya uchochezi ambayo ina dhamana, lakini miezi mitatu leo hajaweza kupata dhamana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huo huo tuna Mbunge mwingine wa Kilombero, Mheshimiwa Lijualikali ambaye anatumikia kifungo cha miezi sita katika Gereza la Ukonga kule Dar es Salaam na kazi ngumu; wakati huo huo, tuna zaidi ya Madiwani sita wa Chama cha CHADEMA ambao wamefungwa kwa makosa yenye misingi ya kisiasa; tuna viongozi kama Mwenyekiti wa Chama wa Mkoa wa Lindi aliyefungwa miezi nane kwa kufanya kazi yake ya kisiasa. Tuna viongozi wa ngazi mbalimbali zaidi ya 215 aidha wamefungwa ama wanaendelea na mashtaka mbalimbali katika maeneo mbalimbali ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona namna Serikali inavyotumiwa mawakala na vibaraka wake kukigawa na kukidhoofisha Chama cha Wananchi (CUF) ikiwemo kumtumia Msajili wa Vyama vya Siasa kudhoofisha Upinzani. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu, je, maadam Mheshimiwa Rais alishatangaza kwamba kusudio lake ni kufuta vyama vya upinzani kabla ya mwaka 2020, haya yanayoendelea katika Awamu ya Tano ambacho ni kinyume na utamaduni na mazoea yetu kama Taifa, ni sera au utekelezaji wa sera hiyo ya kuua upinzani; na ni sera chini ya Serikali yako na Mheshimiwa Magufuli?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nikanushe kwamba Mheshimiwa Rais hajawahi kutangaza kuvifuta Vyama Vya Upinzani.
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, kama ambavyo Mheshimiwa Naibu Spika umesema kwamba Watanzania wote wanajua kwamba nchi hii inaongozwa kwa sheria, kanuni na taratibu, lakini pia tunajua katika kuendesha nchi tunaendesha kwa mihimili mitatu. Iko Serikali, Mahakama na Bunge. Hakuna mhimili unaoweza kuingilia mhimili mwingine. (Makofi)
Tatu, Watanzania wote wanajua kwamba jambo lolote ambalo liko Mahakamani haliwezi kuzungumzwa mahali pengine popote. Kwa hiyo, siwezi kutumia nafasi hii kuzungumzia mambo yote yaliyoendelea chini ya sheria na yaliyoko Mahakamani. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister