Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 3 Finance and Planning Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2016-11-03

Name

Ritta Enespher Kabati

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Mheshimiwa Waziri Mkuu, hakuna Serikali yoyote duniani ambayo haitozi kodi. Ni lazima tulipe kodi ili tupate madawa, watoto wasome, tupate maji na kadhalika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kipindi kirefu sana, wafanyabiashara wamekuwa wakilalamika kunyanyaswa na baadhi ya Maafisa wa Kodi na wengine wakikadiriwa kodi isiyostahili na mbaya zaidi kuna wazabuni ambao wanaidai Serikali yetu. Je, nini kauli ya Serikali kwa jambo hili?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabati, Mbunge wa Iringa, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, nikiri kwamba nimepata malalamiko na baadhi ya wafanyabiashara katika maeneo mbalimbali. Mimi nimekuwepo kwenye ziara ya kawaida Mkoani Mbeya na kwenye kikao changu na wafanyabiashara, wamewahi kueleza matatizo yanayowapata chini ya chombo chetu cha TRA.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza wao niliwahakikishia, naomba nirudie tena kwamba Serikali hii inaheshimu na kuwathamini wafanyabiashara wote, wawekezaji wote na wadau wote walipa kodi ndani ya nchi hii, kwa sababu maendeleo yetu katika nchi yataletwa na sekta ya wafanyabiashara na wawekezaji wakiwa ndio walipa kodi wakubwa, wazuri nchini na uchumi wetu unategemea sana kodi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo lililopo ndani ya chombo chetu cha TRA, tumeendelea kufanya vikao nao, kuwasisitiza na kuwataka wafuate kanuni na taratibu za ukusanyaji wa kodi na kuwasisitiza watumie lugha zenye busara pale wanapotakiwa kwenda kuonana na mfanyabiashara kuzungumzia jambo lolote au kukusanya kodi wanapofika kwenye duka lake au sehemu yake ya biashara. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nataka niwasihi wafanyabiashara, popote ambako unadhani hutajendewa haki na mtumishi wa TRA; TRA yetu inacho chombo cha nidhamu na maadili cha TRA ambacho kinapokea malalamiko mbalimbali dhidi ya watumishi ambao hawafuati kanuni na hawana maadili katika kutekeleza jukumu lao.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia, mfanyabiashara yeyote, mwekezaji yeyote, mlipa kodi yeyote ambaye pia atakuwa na malalamiko yoyote yale, bado anayo nafasi ya kwenda kwenye chombo chochote cha usalama kutoa taarifa ya jambo ambalo limemkwaza ili pia tuweze kutafuta dawa sahihi ya baadhi ya watumishi ambao hawafanyi kazi yao vizuri kwenye chombo chetu cha TRA.
Mheshimiwa Naibu Spika, nirudie tena kuwahakikishia wafanyabiashara, wawekezaji na walipa kodi wote, Serikali hii itaendelea kuwapa ushirikiano wa dhati. Serikali hii ambayo sasa tunahitaji kupanua Sekta za Biashara itaendelea kuwaunga mkono kwenye jitihada zenu za kibiashara ili tuweze kupata mafanikio ya maendeleo na kuinua uchumi wetu katika Taifa letu. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister