Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 3 Finance and Planning Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2016-11-03

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Nampongeza kiongozi wa Upinzani Bungeni Mheshimiwa Freeman Mbowe kwa swali zuri ambalo wewe mwenyewe Naibu Spika, umesaidia kuiua CCM humu ndani. Watu wataamini hizo hela mmekula, bora ungeacha ajibu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa naomba nimwulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu. Nitatumia maneno ambayo watawala wanapenda kuyasikia kwamba Serikali hii haijafilisika kabisa na Serikali hii ina mikakati mizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi katika Ubunge wangu wa muda mfupi huu, ile Sheria ya Mfuko wa Jimbo ndiyo sheria ambayo nimeona imekaa vizuri kweli kweli kwa sababu ni fedha ambazo Mbunge anapewa kwa taarifa tu zinaingia kwenye Halmashauri halafu Kamati yake inakaa, miradi inaibuliwa halafu wanapanga inaenda kwa wananchi moja kwa moja, Mbunge hagusi hata shilingi mia.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama Serikali haijafilisika, tangu bajeti ya Serikali yenu hii ya Awamu ya Tano imepitishwa, Waheshimiwa Wabunge hawajapewa fedha hii ya Mfuko wa Jimbo. Sasa naomba unieleze, kama Serikali haijafilisika, Waheshimiwa Wabunge wameahidi miradi mbalimbali katika maeneo yao ya kiuongozi na wananchi wakawa wanasubiri miradi ile, Waheshimiwa Wabunge wanaonekana waongo kwa sababu fedha hazijaenda na Wabunge hawawezi kufanya maamuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Waziri Mkuu, nini kauli yako juu ya hili? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwita kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nataka nimwambie kwamba Serikali hii haijafilisika. Mfuko wa Jimbo wa Mbunge ni miongoni mwa fedha zilizoandaliwa kwa bajeti ambayo tuliipitisha mwezi Julai, lakini Mfuko huu unapelekwa mara moja kwa mwaka kwenye Majimbo yetu. Nawe ni shahidi kwamba toka tumemaliza Bunge sasa tuna miezi mitatu. Bado tuna miezi kama saba ili kuweza kuhakikisha kwamba fedha yote tuliyokubaliana hapa inaenda kwenye maeneo hayo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yapo mambo yana kipaumbele chake, yapo yale ambayo yanaweza kutekelezwa ndani ya mwaka mzima, lakini nataka nikukumbushe kwamba mfumo wa fedha zetu ni cash budget, tunakusanya halafu pia tunapeleka kwenye miradi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimpe Mheshimiwa Mbunge faraja kwamba suala la Mfuko wa Jimbo bado unatambulika na fedha tutazipeleka kwenye Majimbo na Waheshimiwa Wabunge wote tutawajulisha tumepeleka kiasi gani ili sheria zile ziendelee kutumika na Mheshimiwa Mbunge kama Mwenyekiti wa Mfuko wa Jimbo utaendelea kuratibu mipango yako ya Jimbo lako na fedha ambayo tutaipeleka. Kwa hiyo, endelea kuwa mtulivu, fedha tutazipeleka na tutawajulisha Wabunge wote. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Question 1

MHE. MWITA M. WAITARA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana. Kwanza niseme tu kwamba majibu ya Mheshimiwa Waziri Mkuu yamenishtua; amesema fedha inatolewa mara moja kwa mwaka na wengine wanasema ni mara mbili kwa mwaka.
Mheshimiwa Naibu Spika, nataka tu nijue, mimi ni Mbunge wa Jimbo la Ukonga; niliposoma sheria inasema unapogawanya zile fedha inabidi kuangalia population na mazingira ya Jimbo. Kwa mfano, Jimbo la Ukonga na Jimbo la Segerea, mwenzangu anapokea shilingi milioni 33, mimi napokea shilingi milioni 16. Ni kama mara mbili yangu, lakini wananchi wa Segerea ni karibu 600,000; mimi watu wa Jimbo langu tumezidiana kama watu 50,000 hivi.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri Mkuu upo tayari kusimamia Serikali yako ili kuangalia hali halisi ya majimbo yetu yalivyo. Mtu mwenye mazingira magumu ya Jimbo lake apate fedha nyingi zaidi kwa sababu hata mahitaji ya miundombinu ni mingi zaidi kuliko Majimbo mengine? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba kumejitokeza matatizo kidogo kwenye Halmashauri zenye Jimbo zaidi ya moja na hasa Majimbo yale ambayo yameanzishwa kipindi hiki cha karibuni. Jukumu la Serikali kupitia Wizara husika ni kuendelea kufanya sensa kabla hatujaanza kuzipeleka fedha ya kutambua idadi ya wananchi walioko kwenye Jimbo husika baada ya kuwa Halmashauri yote kuwa ina Majimbo zaidi ya moja; tuweze kujua kila Jimbo lina wananchi wangapi ili sasa tunapopeleka fedha, tupeleke tukiwa tuna maelekezo hasa kwenye Halmashauri zenye Majimbo zaidi ya moja, kwamba kila Jimbo sasa lipate mgao kiasi gani?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mwita niseme, tatizo lililoko Ukonga na eneo la Segerea litakwisha kwa sababu kazi hiyo inafanyika ndani ya Wizara kabla hatujaanza kupelekka fedha.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaamini kama Jimbo lako lina idadi kubwa ndilo ambalo litapata fedha nyingi kulinganisha na Jimbo lingine ambalo lina idadi ndogo ya wananchi ili sasa kila Mbunge kwenye eneo lake aweze kupanga mipango ya maendeleo kwa fedha ambayo imekuja inayolingana na idadi ya wakazi kwenye eneo hilo.