Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2023-09-07

Name

Jackson Gedion Kiswaga

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kalenga

Primary Question

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi kumwuliza Waziri Mkuu swali. Kwa kuwa tabia za watu za uharibifu wa mazingira zimesababisha kuwa na nchangamoto za ukosefu wa mvua na hivyo kuhatarisha pengine usalama wa chakula katika Taifa letu na hivyo kusababisha pia mabadiliko ya tabianchi: Je, ni mpango gani wa Serikali sasa kuzuia kabisha shughuli za kibinadamu kwenye milima yote na vilima vyote ili sasa tuwe na mvua za uhakika na hivyo kulifanya Taifa liendelee kuwa imara katika emneo hilo? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, suala la uhifadhi wa mazingira Serikali yetu tumeliwekea nguvu kwa sababu tunataka tulinde mazingira haya kwa misitu yetu, mito na vyanzo vya maji kwa lengo la kufanya Taifa hili kuwa endelevu na kutoa fursa za upatikanaji wa maji na pia tupate mvua za kutosha kupitia misitu.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Makamu wa Rais eneo la Mazingira wamefanya kazi kubwa na wanaendelea kufanya kazi kubwa kukabiliana na uharibifu wa mazingira. Kwanza ziko sheria zinasimamia uhifadha wa mazingira ambapo pia wenyewe tumeendelea kushirikisha mpaka kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa; mkoani, wilayani na kwenye halmashauri zote na vijijini ambapo ndiyo misitu ilipo, kila mmoja ashiriki katika uhifadhi wa mazingira.

Mheshimiwa Spika, pia tumeendelea kutoa elimu kwa Watanzania kuhusu umuhimu wa uhifadhi wa mazingira, misitu yetu pamoja na vyanzo vya maji kwa sababu vyote hivi vina umuhimu mkubwa kwenye maisha ya kila siku ya binadamu. Hata hivyo, tumekuwa tunashirikisha taasisi mbalimbali za umma na zile za binafsi kwenye uhifadhi wa mazingira na kwenye eneo hili tunaungwa mkono sana. Malengo yetu ni kukabiliana na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi.

Mheshimiwa Spika, kubwa zaidi ni programu mbalimbali zilizoko ndani ya Serikali zinazosimamia uhifadhi wa mazingira kwenye milima hiyo ya miinuko, kwenye mabonde na maeneo yote ambayo yana misitu ambayo tunaitumia kwa ajili ya kuhifadhi mazingira yetu. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Watanzania, kwanza kuona umuhimu wa uhifadhi wa mazingira kwa maslahi yetu.

Mheshimiwa Spika, mabadiliko ya kupatikana kwa mvua yanatokana na uharibifu wa mazingira ambao sasa unaendelea; pia ukosefu wa maji kwenye maeneo ambayo tulikuwa tunatarajia tupate maji kama vyanzo ili tujenge miradi ya maji inatokana na uharibifu wa mazingira. Madhara haya na madhara mengine ndiyo yanasababisha sasa kuwa na mabadiliko ya majira, kuhamahama kwa wanyama kutoka kwenye maeneo yao kuhamia kwenye maeneo mengine wakitafuta maji na aina nyingine yoyote ya usumbufu ambao tunaupata.

Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge, kwa hiyo, nataka niwakikishie kwamba Serikali inao mpango huo wa kuhifadhi mazingira, kupitia Ofisi ya Makamu wa Rais na tumeipeleka hiyo mpaka TAMISEMI, tusimamie kwa pamoja tuhakikishe kwamba nchi yetu tunakabiliana na uharibifu wa mazingira. Kwa kufanya haya, tunaweza sasa tukaokoa mazingira yetu na tukaanza kunufaika na uwepo wa misitu hii, vyanzo vya maji na aina nyingine yoyote ya uhifadhi ambayo tumeiwekea sheria, na tutaendelea kuimarisha sheria zetu na kusimamia sheria zetu. Vile vile taasisi zote ambazo zinahusika katika uhifadhi zisimamie kikamilifu. Huo ndiyo mkakati wetu tulionao ndani ya Serikali, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister