Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2023-09-07

Name

Zainab Athuman Katimba

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Spika ahsante, zao la chikichi ni zao ambalo linaweza kuleta ukombozi mkubwa kwa Taifa katika kujitosheleza katika uzalishaji wa mafuta ya kula nchini, hasa ukizingatia kwamba kujitosheleza katika uzalishaji wa mafuta ya kula nchini kutasaidia kupunguza changamoto ya nakisi ya urari wa malipo inayotokana na uagizaji wa bidhaa nyingi kutoka nje ya nchi.

Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha kunakuwa na programu endelevu ya kukuza zao la chikichi katika Ukanda wa Ziwa Tanganyika ikiwa ni pamoja na maeneo mengine ya nchi ambapo zao la chikichi linastawi? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Katimba, Mbunge, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amezungumzia zao la mchikichi, ni kweli kwamba Serikali yetu tulishaanza mkakati wa kulirudisha zao hili kwa wakulima kwa kulima kisasa na kupata mbegu bora ili tuongeze uzalishaji ukilinganisha na uzalishaji tuliokuwanao awali ambao ulikuwa unatumia mbegu ambazo hazizalishi na kutoa mafuta mengi, lakini pia hata hamasa ya kilimo cha chikichi ilipungua sana.

Mheshimiwa Spika, tulipokuwa tunaanza kurudisha zao hili liwe kwenye mpango wetu wa kiserikali, inatokana na mahitaji makubwa ya mafuta hapa nchini. Kwa hiyo, mkakati wa kupata mafuta ya kula hapa nchini unatokana na mkakati wa ndani kwa mazao hayo ya chikichi na mazao mengine kama vile alizeti na mazao yote yanayotoa mafuta.

Mheshimiwa Spika, mkakati wa Serikali katika kulipanua zao hili, kwanza tumeimarisha kuwa na kituo cha utafiti, na kule Kigoma tumejenga kituo cha utafiti na ndicho ambacho kimeleta mafanikio makubwa kwa kupata mbegu yetu wenyewe Watanzania kutoka kwenye vituo vyetu. Ndiyo hiyo ambayo tumeipanda na sasa inaendelea vizuri na tunafanya ukaguzi wa mara kwa mara na tumethibitisha kwamba mbegu yetu inafanya vizuri.

Mheshimiwa Spika, pia utafiti huu unakwenda sambamba na kutafiti udongo unaoweza kumea mchikichi na kupata matunda, siyo tu kwa ukanda wa Ziwa Tanganyika bali na maeneo mengine yote nchini ili tulipande zao hili, liwe pana, na watu wanaoshughulika na kilimo waweze kuingia kwenye sekta hiyo wakiwa na uhakika kwamba wanapanda mchikichi kwenye ardhi ambayo inaweza kuzalisha zaidi. Hiyo ni moja.

Mheshimiwa Spika, pili, tumeanza kampeni ya zao hili na sasa imeanza kuleta matunda. Tunaona pia Mkoa wa Tabora wanalima, tumeona Mikoa ya Pwani, Mkoa wa Pwani wenyewe, Dar es Salaam, ndiyo twende Lindi, Mtwara, tunaona maeneo yote yanayopanda zao la minazi pia tunaambiwa yanaweza kustawisha zao la mchikichi. Huu ni mpango wa kupanua zao hili ili tupate mazao mengi zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunapoanza na mkakati huu kupitia kituo chetu cha utafiti na kuzalisha mbegu nyingi, tumeanza kutoa mbegu inayozalishwa bure kwa wakulima katika kipindi kisichozidi mwaka mmoja ili kupanua wigo wa watu ambao wanaanzisha kilimo hiki ili waweze kupanda zao hili la mchikichi, huku pia tukiimarisha uwekaji wa viwanda vidogo vidogo kwa ajili ya wachakataji, kwa sababu baada ya kuwa tumezalisha, tunahitaji sasa tuone matokeo. Hii itasaidia watu wengi kuingia kwenye kilimo na kuwezesha kulima zao hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, mkakati huu wa kukuza zao hili tunausimamia toka tulipoanza kulima zao hili Kigoma, na Mkoa wa Kigoma ni watu ambao wameanza mara moja kulilima zao hili na mafanikio tunayaona na tunaona mikoa mingine nao pia wanachukua miche na upandaji tunaona maendeleo yake. Kwa hiyo, tunataka tuhakikishe kwamba zao la chikichi sasa linaanza kuchangia upatikanaji wa mafuta ndani ya nchi na mazao yake mengine na kunufaisha yeyote ambaye anaingia kwenye kilimo cha chikichi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na wakulima wa zao la chikichi kwamba Serikali itaendelea kusimamia maendeleo ya zao hili na hapo baadaye litakapokuwa kubwa tunaweza tukaliundia chombo chake cha usimamizi wa zao hili ili pia liweze kusimamiwa kwa ukaribu zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, malengo yetu ni kwamba tunatoa fursa kwa Watanzania wanaotaka kulima kilimo wawekeze kwenye mashamba makubwa, wanaotaka kujenga viwanda na tumehusisha pia na taasisi za umma na taasisi binafsi kulima zao hili. Kule Kigoma tuna Magereza, Magereza zote zinalima chikichi, shule za msingi nyingi zimekuwa na mashamba yao, wanalima chikichi, pia Jeshi la Kujenga Taifa, JKT Bulombora nao wana shamba kubwa zaidi ya ekari 4,000 na tunaendelea kuhamasisha taasisi zote zilime zao hili lilete manufaa makubwa.

Mheshimiwa Spika, niwahamasishe Watanzania kulima mchikichi kwa faida yao. Tulime mchikichi kwa ajili ya kupata mafuta mengi, tulime mchikichi kwa sababu na yenyewe inatoa sabuni na bidhaa nyingine ambazo pia zinaleta faida kwenye zao hili.

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo mkakati wa Serikali wa kupanua zao hili. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister