Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2023-09-07

Name

Kilumbe Shabani Ng'enda

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Primary Question

MHE. KILUMBE S. NG’ENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, sera yetu ya viwanda hapa nchini imetuwezesha kupata viwanda vingi sana na kuwafanya Watanzania watumie bidhaa nyingi ambazo zinatengenezwa hapa nchini. Hata hivyo, sera hii bado haijapiga hatua kubwa katika viwanda vinavyoongeza thamani ya mazao ya wakulima, wafugaji na wavuvi. Tunataka tuone viwanda vya maziwa, vya nyama, tunataka kuona viwanda vya kusindika samaki, dagaa, na viwanda vya kusindika matunda.

Je, ni nini mpango wa Serikali katika kuongeza viwanda vya kusindika au kuongeza thamani ya mazao ya wakulima? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ng’enda Kilumbe, Mbunge wa Kigoma Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali yetu imeendelea kutafuta mbinu mbalimbali za kuwawezesha Watanzania wanaojishughulisha kwenye sekta zote zinazozalisha mali na kuongeza uchumi, kuhakikisha kwamba tunaongeza thamani ili mapato yawe makubwa zaidi ikiwemo na sekta ambazo Mheshimiwa Mbunge amezieleza, Sekta ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi.

Mheshimiwa Spika, sekta hizi zimekuwa na manufaa makubwa kwa sababu sekta hizi ndiyo zina uwezekano wa kuwa na viwanda vingi kwa sababu zinakuwa na malighafi nyingi, na kwa hiyo, mkakati wa Serikali kuongeza viwanda zaidi ya viwanda tulivyonavyo, ni kuhakikisha kuwa na hili tumeshalifanya la kujenga mazingira mazuri ya uwekezaji hapa nchini ili kuweza kuwavutia wawekezaji wanaotaka kujenga viwanda, awe Mtanzania au yeyote kutoka nje ya nchi kwa maslahi ya Taifa.

Mheshimiwa Spika, pia tumefungua wigo wa kuhakikisha kuwa, wawekezaji wote wanapokuja nchini tunawahakikishia uwekezaji wao kuwa salama. Kwa hiyo suala la usalama kwa wawekezaji wetu tumelipa nafasi kubwa ili kuwakaribisha walio wengi sana. Hata hivyo, tumeimarisha miundombinu inayowawezesha wafanyabiashara wanaotaka kujenga viwanda kuendesha viwanda vyao na kupata faida, kama vile barabara na Watanzania mnaona barabara zote nchini zimejengwa na zinaendelea kujengwa, reli lakini pia njia ya anga, tumeshanunua na ndege ya kupeleka mazao nje ya nchi. Hii yote ni kuvutia wawekezaji wetu, hata pia ukanda wa bahari na maziwa tumeongeza meli ili kuwezesha kusafirisha bidhaa zao kwa ajili ya kufuata masoko. Uboreshaji wa mazingira haya ya miundombinu unamuwezesha kumpa uhakika muwekezaji kujenga kiwanda popote nchini ili aweze kutumia malighafi tulizonazo aweze kufanya biashara yake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, tulikuwa tunaangalia wafanyabiashara wengi, wawekezaji wengi wa viwanda wanakwazwa wapi? Tukagundua kwamba tulikuwa na tozo nyingi sana za uwekezaji. Tumepunguza tozo ili kumuwezesha yeye kufanyabiashara na kupata faida na bado mkakati wetu wa kufanya mapitio ya mara kwa mara ya uwekezaji wetu unafanywa kuvutia wawekezaji hao.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nitoe wito tena kwa Watanzania wenye uwezo kujenga viwanda ndani ya nchi, malighafi tunazo kwa sababu Sekta ya Kilimo imepata mabadiliko makubwa, Mifugo nako pia tuna malighafi za kutosha na uvuvi nako pia tumeimarisha uvuvi bora na wa kisasa kwa lengo la kupata malighafi nyingi za kuendesha kwenye viwanda vyetu, lakini pia tunajaribu kuhakikisha kwamba tuna tunasikiliza kero za wawekezaji. Hii inatoa fursa sasa ya Mwekezaji kufanya maamuzi kuja nchini na ndiyo kwa sababu wakati wote tumekuwa na maonyesho ya viwanda, maonyesho ya kilimo ili kuwahakikishia kwamba viwanda vina nafasi vilivyopo na vile ambavyo vinakuja, lakini kwenye maonesho ya mazao kuonesha uwepo wa malighafi hapa nchini. Tunaendelea kufanya haya kwa kutoa wito na kufanya maboresho ya maeneo yote niliyoyatamka ili kukaribisha viwanda zaidi hapa nchini.

Mheshimiwa Spika, huo ndiyo mpango wetu ambao tunao wa kuwezesha kuongeza viwanda viweze kuleta faida nchini na sisi tunaamini kwamba tukiwa na viwanda kwanza tunatengeneza ajira kwa Watanzania, mbili, tunapata kodi ya hawa wawekezaji wanalipia, tatu tunahakikisha kuwa huduma mbalimbali zinazohitajika viwandani wale majirani wananufaika nazo. Hayo yote ni manufaa ambayo tunayapata na kwa hiyo wito wako uliotokana na swali lako, tutaendelea kuusimamia na kuyasimamia hayo maboresho tunayoyafanya kwa lengo la kuvutia wawekezaji zaidi wa kujenga viwanda hapa nchini. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister