Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2023-09-07

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nishati ya mafuta ni nishati ambayo ni muhimu sana kwa Taifa letu, kwanza kwa sababu ni sehemu ya ulinzi na usalama wa nchi, lakini pili pia ni sehemu ambayo inachangia kwa mawanda mapana shughuli zote za kiuchumi katika nchi yetu. Lakini miezi ya hivi karibuni kuanzia Mwezi wa Saba, Mwezi wa Nane na hata Mwezi huu wa Tisa kumekuwa na sintofahamu kwenye eneo hili la sekta ya nishati. Upatikanaji wa mafuta umekuwa ni wa mashaka pia bei zimekuwa zikibadilika bila ya kuwa na mpangilio maalum. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika hali ambayo ni ya kushangaza zaidi ni kwamba wiki moja ama mbili kabla ya kutangazwa bei ya mafuta kama utaratibu ulivyo kwamba kila Jumatano ya kwanza ya mwezi mpya bei ya mafuta zinatangazwa, mafuta huwa hayapatikani, bei ikishatangazwa tayari mafuta yanaanza kupatikana.

Mheshimiwa Spika, nataka kufahamu ni upi mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba Taifa linakuwa na mafuta wakati wote, lakini pia kuhakikisha kwamba yanapatikana kwa bei ambayo Watanzania kote nchini wanaweza kuimudu? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza ninakiri kwamba tunazo changamoto za upatikanaji wa mafuta nchini, kwa sababu baadhi ya vituo kwenye maeneo mbalimbali vimekuwa vikikosa mafuta na Watanzania wanaohitaji huduma hii maeneo kadhaa tumeona wakiwa wanalalamika kukosekana kwa mafuta.

Mheshimiwa Spika, ziko jitihada kadhaa zinafanywa na Serikali kupitia mifumo yetu ya upatikanaji wa mafuta, Wizara imekuwa ikifanya jitihada pia za kuona upatikanaji wa nishati hii unakuwepo, pia hata Kamati ya Bunge ya Nishati imekaa mara kadhaa na Wizara kuona mwenendo wa upatikanaji wa nishati hii. Nasi tunajua nishati hii ina msaada mkubwa kwenye maeneo mengi na ndiyo inasaidia pia kufanya shughuli za kiuchumi ziweze kwenda.

Mheshimiwa Spika, kufuatia mabadiliko ya Mheshimiwa Rais aliyoyafanya juzi, tumeanza kumwona Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu akifanya vikao kadhaa ndani ya Wizara kukutana na wadau. Sasa kwa kuwa ameshaanza hii kazi, niendelee kumuagiza Naibu Waziri Mkuu kushughulikia hili. Muhimu zaidi nishati yenyewe ipatikane nchini, suala la bei tunajua bei zinabadilika wakati wowote, lakini kwanza nishati ipatikane kwenye vituo vyote na maeneo yote nchini. Pili Watanzania wapate hii huduma na upatikanaji huu ni muhimu kuhusisha pia taasisi zote za mafuta, EWURA na taasisi nyingine zote wale wanunuaji wa mafuta kwa bulk, lakini pia Taasisi ya Ununuaji wa Mafuta tutengeneza kikao kikubwa na Wizara kadhaa zinazohusika, Wizara ya Fedha, Ofisi ya Uratibu, Ofisi ya Waziri Mkuu mkae pamoja, muone namna ya upatikanaji wa mafuta, suala la bei tutaanza kuliangalia hapo baadae kwa sababu bei zinabadilika kutegemeana na upatikanaji.

Mheshimiwa Spika, pia tupanue wigo wa waagizaji wa mafuta ili tuwe na mafuta mengi nchini kwa usalama wa Taifa letu. Kama hili litafanyika ndani ya wiki moja tutakuwa tumeshapata majibu na tutawapa taarifa Watanzania, lakini tutahakikisha kwamba nishati hii ya mafuta inapatikana na Mheshimiwa Naibu Waziri Mkuu atashughulikia hilo. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister