Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 10 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2023-02-09

Name

Ng'wasi Damas Kamani

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NG'WASI D. KAMANI: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Mfuko wa Maendeleo ya Vijana ulio chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu ulianzishwa kama namna mojawapo ya kutatua changamoto ya ajira kwa vijana na chanzo kikuu cha mapato katika mfuko huu ni bajeti inayotengwa na Serikali kupitia Bunge hili tukufu na kwa miaka saba mfululizo, mfuko huu umekuwa hautengewi fedha zozote. Mwaka 2022 mfuko huu umetengewa shilingi bilioni moja ambayo inatakiwa kwenda kwa vijana katika Halmashauri zote 185 nchi nzima. Fedha hizi ni ndogo, hazitoshi na hivyo hata impact ya mfuko huu haionekani kwa vijana. Sasa nini mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba inatafuta vyanzo vingine vya mapato katika mfuko huu ili kuutunisha na kuuongezea tija zaidi? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba tu ridhaa yako nimjibu Mheshimiwa Ng’wasi na nataka nimjibu kwa sababu ameuliza swali ambalo liko ofisini kwangu na nalifahamu vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu inayo Wizara inashughulikia vijana na kwenye eneo hili, ziko programu mbalimbali za uwezeshaji kwa vijana wetu na tumeanzisha na mfuko huo wa vijana.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge amesema kwa miaka 7 haujatengewa fedha, lakini katika kipindi hiki hiki tulishatenga fedha zaidi ya bilioni moja, kumbukumu zangu nilizonazo ofisini zinaonesha mwaka 2017 tulitenga bilioni moja, hazitoshi kwa mahitaji ya vijana nchini, tukaongeza tena bilioni nane, tukawa na bilioni 1.8 na tulishaanza kuzitoa. Tunatoa kwa vijana kwenye halmashauri zetu ambao wanakidhi vigezo na vigezo kukidhi vigezo ni moja kwanza ufahamike na Ofisi ya Halmashauri, uko wapi? Unafanya nini ili unapopata ile fedha, basi Ofisi ya Halmashauri ambayo inaratibu vijana iwe inafahamu huyu kijana yuko wapi na kwa kuwa sehemu kubwa inaweza kuwa ni mikopo au support lakini tujue kwamba kama ni mkopo unaweza kuurejesha.

Mheshimiwa Spika, sasa nini kinafanyika? Kwanza tumeunda mfuko maalum huu mfuko ambao tumeunda na tunao mwongozo wa kuendesha mfuko huo. Na mfuko huu, mbali ya Serikali lakini pia huwa tunatoa fursa kwa wadau kuuchangia na sasa tumeanza kuona taasisi mbalimbali ambazo zinasaidia Serikali yetu katika kukuza uwezo wa vijana uweze ku-support.

Nini Ofisi ya Waziri Mkuu imefanya, baada ya kuona kwamba kiwango hiki hakitoshi? Kwa kuwa Ofisi ya Waziri Mkuu inalenga kuwawezesha vijana kumudu, kufanya shughuli mbalimbali za kiuchumi, sisi tumeanzisha programu ya uanangezi, programu ambayo inawachukua vijana na kuwapeleka kwenye vyuo mbalimbali nchini, ili kupata ujuzi ambao utamuwezesha yeye mwenyewe kujiajiri. Tunawapeleka VETA, tunawapeleka vyuo ufundi binafsi, lakini tunawapa pia mafunzo ya huduma, utoaji huduma, kuwapeleka mahotelini namna ya kutoa huduma kwenye hoteli mbalimbali na anapomaliza kozi yake ya miezi sita, ambayo inagharamiwa na Serikali anakuwa tayari anaweza kujiajiri au kuajiriwa na sekta mbalimbali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, programu hizi zipo nyingi na tunaendelea kuziratibu na nikuhakikishie najua Mheshimiwa Ng’wasi ni Mbunge na unawakilisha vijana tunao mpango wa kuhakikisha vijana hawa wanakuwa na uwezo, lakini wanakidhi vigezo vya kuweza kupata support kupitia mfuko huu.

Mheshimiwa Spika, lakini hatujaishia hapo tu, Serikali tumeendelea pia kutoa maagizo kwa Halmashauri za Wilaya, ule mfuko unaokopesha wa asilimia nne, wenye kipengele cha vijana cha asilimia nne nao pia wananufaika, na sasa nishauri ili waweze kunufaika waunde vikundi kwenye maeneo yao. Mmoja mmoja ni ngumu, unaweza kukosa kufikia vigezo, lakini mkiwa kikundi inakuwa rahisi zaidi mtafanya shughuli ya pamoja. (Makofi)

Kwa hiyo mfuko wa halmashauri wa asilimia nne nayo inasaidia katika halmashauri zote katika kutambua vijana na kuwa-support ili waweze kufanya shughuli zao kwa lengo la kuongezea uchumi wao. Kwa hiyo, programu ya Ofisi ya Waziri Mkuu, programu iliyoko Ofisi ya Rais, TAMISEMI hizi zote kwa pamoja, lakini pia michango tuliyopata kwa wadau yote hii inaimarisha katika kuwawezesha vijana kufikia katua na malengo waliyojiwekea, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister