Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 9 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2022-11-03

Name

Ally Mohamed Kassinge

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Primary Question

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, ahsante, kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu. Swali litajikita katika eneo la zoezi la utambuzi wa mifugo kwa kutumia hereni za kielektroniki.

Mheshimiwa Spika, ninafahamu kwamba Serikali ilipoanzisha zoezi hili ilikuwa na nia njema kama ambavyo Mheshimiwa Waziri ameieleza lakini sisi wananchi pamoja na hayo ambayo Mheshimiwa Waziri Mkuu ameyaeleza tunatambua pia kwamba zoezi hili lingepunguza kwa kiwango kikubwa migogoro ya wafugaji dhidi ya watumiaji wengine wa ardhi, kwa sababu mifugo ingekuwa imetambuliwa.

Mheshimiwa Spika, sasa wakati Serikali imesitisha zoezi hili ili iweze kufanya tathmini kwa miezi mitatu; nini mkakati wa Serikali wa muda mfupi na wa muda mrefu wa kuhakikisha kwamba uingizaji holela wa mifugo hautoendelea na hautoweza kuathiri na kuleta migogoro baina ya wafugaji na watumiaji wengine wa ardhi?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba yako matatizo kwenye sekta ya ufugaji ambapo kwa sasa tunaona kuzagaa holela kwa mifugo yetu, lakini pia mifugo mingi kuingizwa kwenye vyanzo vilivyohifadhiwa kisheria na kusababisha madhara mengine kama ambavyo sasa tumeona vyanzo vingi vinakauka.

Mheshimiwa Spika, kusitisha kwa miezi mitatu kutaiwezesha Wizara sasa kuweka mkakati thabiti kwanza kuhakikisha kwamba wanakutana na wadau na kuelimisha namna nzuri ya ufugaji kisasa kama alivyotamka kwenye taarifa; na pili, kushirikisha mamlaka za Serikali za Mitaa kwa maana ya Ofisi ya Mkuu wa Mkoa na Ofisi ya Mkuu wa Wilaya kutambua maeneo yote yenye mifugo na mipaka yao ili sasa lengo la kuweka hereni ambapo moja kati ya malengo ya kuweka hereni yaliyokusudiwa ni kuhakikisha kwamba tunapunguza kuhamahama kwa mifugo hii kiholela kutoka eneo moja mpaka eneo lingine, kwa sababu hereni inatambulisha mahali mfugo ulipo kwa sasa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwa utaratibu huu tutakuja kujipanga vizuri na kesho kutwa tuna kikao cha Mawaziri wote wenye sekta zinazohusu mifugo, maji, mazingira pamoja na ardhi, pamoja na Mamlaka za Serikali za Mitaa hapa Dodoma kuweka mkakati wa kudhibiti hali hiyo. Hiyo ndiyo moja kati ya njia ambayo tumeamua ili tuweze kufikia hatua nzuri ya kuelimisha pia na wafugaji umuhimu wa kufuga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo mnakumbuka wakati tunaendesha zoezi la wanaohama kwa hiari Ngorongoro, na watu wa Loliondo kupisha lile eneo na kuwaweka mahali pazuri na upimaji wa vijiji vyao, tuliiagiza Wizara itumie vizuri eneo la Msomera kuwa ni eneo la ufugaji kisasa la kimkakati kama pilot area ili wafugaji wengine wapate kujifunza kutoka Msomera.

Mheshimiwa Spika, wakati Wizara inaendelea na zoezi hilo la kuratibu vizuri pale Msomera, tunataka sasa mfumo huo uhamie kwenye Halmashauri nyingine zote nchini ili ufugaji sasa uwe na tija, wafugaji watambulike, mifugo tuitambue, tuwasaidie kutohama kwa umbali mrefu unaosababisha mifugo kupata shida, kutafuta malisho na huku Serikali ikijipanga kujenga maeneo ya kunyweshea na majosho. Huo ndiyo mkakati wa Serikali.

Additional Question(s) to Prime Minister