Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2022-02-10

Name

Tarimba Gulam Abbas

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kinondoni

Primary Question

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi. Swali langu linahusu huduma ya umeme.

Mheshimiwa Spika, natambua, nathamini na vilevile naipongeza Serikali kwa juhudi kubwa sana za kuhakikisha kwamba Taifa hili linakuwa na umeme wa uhakika. Nafahamu vilevile kwamba kumekuwa na initiatives nyingi za Serikali ikiwemo hii ambayo imetolewa tarehe 30 Juni, 2014 ambayo ni ya Electricity Supply Industry Reform Strategy and Roadmap. Katika utafiti huo inaonekana kuna matatizo makubwa ya generation, transmission pamoja na distribution.

Mheshimiwa Spika, sasa TANESCO inaonekana kuhemewa na kazi hii hasa kwa kuwa tunakwenda kuwa na umeme mkubwa kutoka Mwalimu Nyerere Hydropower Supply. Kwa hali hiyo, Serikali haioni kwamba muda muafaka sasa wa kwenda kuifumua TANESCO ili tuwe na makampuni matatu ya generation peke yake, transmission peke yake pamoja na distribution kama ilivyo katika nchi nyingine na hata majirani zetu wa Kenya, Uganda, South Africa na kwingineko? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba ridhaa yako angalau hili eneo la mwisho naweza kulitolea ufafanuzi kama ambavyo Mheshimiwa Abbas Tarimba, Mbunge wa Kinondoni, mwanamichezo alivyouliza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, shirika letu la umeme nchini linafanya kazi kubwa sana. Kazi hiyo kubwa ambayo inafanywa kwa sasa, lenyewe ndiyo linazalisha, lakini TANESCO pia inasafirisha umeme na inafanya kazi ya kugawa. Unapofanya jukumu hili, pia tunaangalia na maslahi ya Taifa, kwamba maeneo haya unaweza ukawa umeyakatakata ukawapa watu tofauti tofauti ikakuletea athari kwenye usalama wa nchi. Pale ambako nchi inahitaji umeme wakati wote, halafu mmoja miongoni mwao anafanya mambo anayoyataka tu, halafu ukashindwa kufikia malengo ya kupeleka umeme kwa wananchi.

Mheshimiwa Spika, tunapokea ushauri wake. Hali tuliyonayo sasa nchini, maeneo yote yanayozalisha umeme tunaendelea kuzalisha umeme. Tuna maeneo ya maji; tunapopata mvua za kutosha kama sasa maji yamejaa, mfano Kidatu na Mtera, tunayo maji ya kutosha na uzalishaji unaendelea. Kwa hiyo, eneo hili halina matatizo. Kwenye eneo la gesi pale Kinyerezi uzalishaji unaendelea. Pia maeneo mengine tunayotumia mafuta yanaendelea pia na uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, TANESCO kwa sasa maeneo yote ya uzalishaji, uzalishaji upo. Changamoto tuliyonayo sasa ni miundombinu iliyopo kwenye maeneo hayo ya uzalishaji. Hii inasababisha pia hata sasa naona kuna baadhi ya maeneo umeme unakatika, lakini ni kwa sababu ya kukosekana miundombinu. Sasa nini mkakati wa Serikali?

Mheshimiwa Spika, moja, tumewapa kazi TANESCO kufanya tafiti. Wanaweza kuja kwenye hatua hiyo ambayo Mheshimiwa Mbunge ameipendekeza. Pale ambapo tutakuwa tumejipanga na tunaona nani tunampa jukumu la kuzalisha, nani anasafirisha lakini pia msambazaji ni nani? Zinaweza kuwa ni taasisi za Serikali ambazo pia lengo lake ni moja. Kwa hiyo, tukifikia hapo kupitia utafiti unaoendelea sasa na Shirika letu la Nmeme Nchini, tutaweza kufikia hatua nzuri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pili, suala la usambazaji, kama ambavyo mmeona Serikali leo ina mkakati wa kupeleka umeme mpaka vijijini, hii hatua tutaifikia kwa sababu tumefanya kazi nzuri sana na leo umeme unapatikana mpaka vijijini. Bado kazi hiyo inaendelea na malengo yetu kufikia Desemba mwaka huu tuwe tumefikia vijiji vyote nchini kupata umeme. Kwa nini? Tuna uhakika wa uzalishaji na bado tunaendelea kutafuta maeneo mengine ya uzalishaji, bado pia shirika letu limetoa nafasi kwa taasisi kuja kuwekeza kwenye uzalishaji. Kwa hiyo, nchi yetu itakuwa na umeme wa kutosha na kwa maana hiyo, eneo la uzalishaji halina matatizo kabisa. Tutajiimarisha pia kwenye eneo la miundombinu ya kwenye eneo la uzalishaji, usafirishaji na ugawaji kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nachukua ushauri wake, tutaufanyia kazi na hivi TANESCO wanafanya kazi hiyo. Tukishakamilisha haya, tutatoa taarifa kwenu Waheshimiwa Wabunge na hasa Mheshimiwa Mbunge ambaye ametoa pendekezo hili, tutakupa mrejesho wa hatua ambayo tutaifikia. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister