Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2022-02-10

Name

Oran Manase Njeza

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana kwa kupata fursa ya kuuliza swali kwa Waziri Mkuu.Mheshimiwa Waziri Mkuu, pamoja na kazi nzuri iliyofanywa na Kamati ya Mawaziri Nane ya kutatua migogoro kati ya hifadhi, hususan TFC na TANAPA, lakini kuna vijiji ambavyo bado havijafikiwa vikiwemo vijiji katika Wilaya yaMbeya. Je, ni lini Kamati hii itarejea kukamilisha hilo zoezi muhimu kwa maeneo yaliyobaki nchi nzima? Nashukuru sana.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, Serikali iliunda timu ya Mawaziri Nane kwa ajili ya kuhakiki vijiji ambavyo vina changamoto au migogoro kati ya vijiji hivyo na hifadhi. Mnatambua Waheshimiwa Wabunge tulipata taarifa za awali za utekelezaji huo na bado kazi hiyo inaendelea.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Njeza anahitaji kujua lini kazi hiyo itakamilika, ili tuweze kwenda kule Mbeya. Nataka nimhakikishie kwamba, kazi iliyofanywa awali ambayo ilibaini vijiji vipatavyo mia tisa kama 75 hivi na kati ya hivyo ilithibitika kuwa vijiji mia tisa na 20 havikuwa na matatizo na bado vilikuwa vinatakiwa kuishi huko kwenye maeneo ambayo tuliyahifadhi, lakini hayana tija. Bado Serikali inakusudia kutambua vijiji kadhaa vyenye migogoro ya aina hii kati ya vijiji na hifadhi, pale ambapo tunaona kwamba, uhifadhi wake hauna tija kwa malengo yaliyokusudiwa, vijiji hivyo vitapata nafasi ya kuendelea kushiriki shughuli za kijamii kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, pindi Kamati itakapokamilisha, tutakuja kutoa taarifa nyingine tena baada ya taarifa ya awali. Sasa, naielekeza Kamati ile pia, kuweka mpango kazi wa kwenda Mbeya Vijijini kuona huko ambako Mheshimiwa Mbunge anasema bado hatujafika, waone vijiji hivyo, lakini pia, aina ya mgogoro uliopo na nini tufanye baada ya kuhakiki. Kwa hiyo, Kamati ya Mawaziri wale nane itakapokamilisha kazi hiyo tutaipata.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito, tunatambua tuna migogoro mingi, iko migogoro ya mipaka kati ya vijiji na vijiji vyenyewe, iko migogoro ya wafugaji na wakulima, bado nielekeze kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa, hususan Waheshimiwa Wakuu wa MIkoa, Wakuu wa Wilaya, lakini tunashuka chini kule kwa Watendaji wa Kata na Vijiji kuhakiki migogoro hii na tujiridhishe kuwa inakamilishwa hukohuko kwenye ngazi hiyo, badala ya kutegemea Mawaziri ambao wako hapa Dodoma wasafiri waje kwenye vitongoji na vijiji badala ya kuwa wamekamilisha kule na Mawaziri wapate unafuu wa kutekeleza hili. Ikifika hatua hiyo ya kila mmoja kuwajibika kwenye nafasi yake hii migogoro itapungua kwa kiasi kikubwa, kama sio kuimaliza kabisa. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister