Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 9 2021-11-11

Name

Ally Mohamed Kassinge

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kilwa Kusini

Primary Question

MHE. ALLY M. KASSINGE: Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kupata fursa hii ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, mradi wa kuchakata gesi unaofanywa katika eneo la Likong’o, Mkoani Lindi ni miongoni mwa miradi ya kimkakati ambayo imekusudia kuinua fursa za kiuchumi katika ukanda wa Kusini na Tanzania kwa ujumla. Nini maelezo ya Serikali kuhusiana na hatua iliyofikiwa ya mradi huu mpaka hivi sasa na Watanzania watarajie nini kutokana na mradi huu. Ahsante sana.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kassinge, Mbunge wa Kilwa Kusini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tuna mradi huu mkubwa wa kimkakati wa LNG ambao uko Mkoani Lindi na kwa bahati nzuri Mheshimiwa Kassinge anauliza swali na anayejibu ni mnufaika nambari moja. Mradi huu hatua tuliyofikia sasa ni nzuri, kwa sababu tayari TPDC wameshiriki kikamilifu kwenye hatua zote za awali ikiwemo na kulipa fidia wananchi wote waliokuwa kwenye eneo lile, wote wameshaondoka. Eneo lile sasa linaandaliwa kulima barabara mbalimbali huko ili kuligawa kwenye plots zile ambazo huduma mbalimbali zitatolewa makazi, sehemu ya kuweka mitambo na maeneo ya utoaji wa huduma nyingine.

Mheshimiwa Spika, hatua nyingine muhimu zaidi ni ya majadiliano ambayo Wizara ya Nishati kupitia Waziri aliyepo sasa ameshaanzisha hiyo timu na wako Arusha kwa sasa wanaendelea ku-negotiate, kufanya majadiliano na yale makampuni. Makampuni yenyewe yako kama manne ambayo yameonesha nia ya kwenda kuwekeza pale eneo la Likong’o pale Mkoani Lindi kwa ajili ya kuchakata gesi.

Mheshimiwa Spika, mradi huu ambao pia utaleta faida kwa Watanzania wote, tumeenda kuwahamasisha, nilikuwa ziarani Mkoani Lindi wiki mbili, tatu zilizopita. Nimetembelea eneo lile la huu mradi, nimekutana na wananchi na nimewaambia wananchi wajipange sasa kunufaika na huo mradi. Kutakuwa na mambo mengi, watakuja watu wengi, kutakuwa na shughuli nyingi, watu wajikite kwenye kilimo, walime mazao yatakayoweza kuuza, watu wafuge watauza, lakini na huduma nyingine hoteli na nyumba za kulala wageni, ziandaliwe. Hizo ndiyo fursa ambazo tunazipata kwa kuwa na miradi mikubwa ya kimkakati kama wa LNG.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Watanzania wategemee mafanikio makubwa kwa mradi huu ambao tayari mchakato wake unaenda katika hatua nzuri ya kwenda kuanza uchimbaji, uanzaji wa kuchimba na kuwekeza kwenye mradi huo. Kwa hiyo kwa ujumla wake miongoni mwa miradi mikubwa nchini ambayo pia ni ya kimkakati umo na mradi huu ambao utatengeneza fursa nyingi ikiwemo na ajira kwa Watanzania wote, kwa Watanzania wale ambao watapata nafasi ya kuajiriwa kwenye eneo lile. Hizo ndiyo fursa ambazo zinatarajiwa na Watanzania kupatikana kupitia mradi huo. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister