Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 8 2021-11-11

Name

George Ranwell Mwenisongole

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kutokana na mabadiliko ya tabianchi na ikolojia, kilimo cha umwagiliaji hakiwezi kukwepwa katika nchi hii. Miaka michache iliyopita Serikali ilitoa mabilioni ya fedha kununua vifaa vya uchimbaji wa mabwawa, lakini mpaka sasa hivi hakuna bwawa hata moja ambalo limechimbwa na hivyo vifaa vimechakaa na kwa sasa ni kama vile spana mkononi. Sasa nini mkakati wa Serikali katika kuhakikisha kwamba mabwawa haya yanachimbwa na kuwekeza fedha zaidi kwenye uchimbaji wa mabwawa ili kukinusuru kilimo chetu na mabadiliko ya tabianchi yanayoikabili nchi hii? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwenisongole, Mbunge wa Mbozi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kwenye sekta ya kilimo, miaka yote nchini tumekuwa tukitegemea sana msimu wa mvua ili kuzalisha mazao yetu. Tumegundua kwamba tunayo fursa ya kutumia mabwawa yawe ya asili au ya kuchimba na kuyajaza maji tukatumia kwa kilimo cha kumwagilia. Tumeweka msisitizo kwenye eneo hili, pale ambapo tulichimba mabwawa mengi kwenye maeneo kadhaa lakini pia kuhakikisha kwamba tunakuwa na maeneo ya kumwagilia pale ambako kuna uwezekano mkubwa au kuna mvua nyingi na mabwawa yanajitengeneza. Serikali inaendelea kusimamia jambo hili kwa sababu tumegundua tukiimarisha kwenye umwagiliaji, tunafanikiwa sana.

Mheshimiwa Spika, Serikali huko awali tulinunua mitambo hiyo ambayo Mheshimiwa Mwenisongole amesema imechakaa. Ni kweli, lakini kwa kuwa sasa tunakisimamia kilimo na maendeleo yake, Wizara ya Kilimo hapa hata walipokuja mbele yetu kuja kuomba kuongezewa bajeti, walieleza waliomba fedha ambayo Waheshimiwa Wabunge wameipitisha kwa ajili ya kuongeza mitambo mbalimbali kwa ajili ya kupanua wigo wa kilimo cha umwagiliaji. Lengo mitambo ile isambazwe kwenye kanda zetu na ifanye kazi ya kuchimba mabwawa kwenye maeneo hayo, yatumike kwa kilimo, lakini wakati mwingine pia na wafugaji watatumia kwa kunyweshea mifugo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali ilishatoa fedha kwa ajili ya kununua mitambo hiyo ili kuendelea kuimarisha mitambo iliyopo kwa kununua vipuli ile iliyoharibika, lakini mipya kwa ajili ya kuendelea kuchimba mabwawa yetu. Kwa hiyo eneo hili tutaendelea kulisimamia kwa sababu tumegundua kwamba lina tija na hasa kipindi hiki ambacho tunaambiwa hali ya hewa ina badilikabadilika, kama tutakuwa na mabwawa na maeneo haya ya kumwagilia, tunaweza tukapata kilimo kizuri tu na tukavuna mazao mengi tu kama ambavyo maeneo yote yenye mabwawa yanavyoweza kufanikiwa.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nimhakikishie Mheshimiwa Mwenisongole kwamba, eneo hili kwa fedha ambayo tumeitoa, tutanunua mitambo na kama haitoshi tutaona uwezekano wa kuongeza ili iweze kufanya kazi ya kuchimba mabwawa katika maeneo yote kadiri ya uhitaji kwenye maeneo haya. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister