Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2021-11-11

Name

Priscus Jacob Tarimo

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa hii nafasi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Sera ya kuwainua wananchi kiuchumi imekuwa na mafanikio sana kwenye ile mikopo inayotolewa na halmashauri kwa ajili ya akinamama, vijana na watu wenye ulemavu. Hata hivyo, kumekuwa na tatizo haswa kwa vijana, vijana wanavyopewa mikopo wakifikisha umri wa miaka 35 vijana wa kike wanaenda kwenye kundi la akinamama, vijana wa kiume wanabaki hawana cha kufanya. Sasa swali langu, ni nini mpango wa Serikali wa kuwainua wanaume kiuchumi kwa sababu sera inasema ni wananchi kwa kufanya moja kati ya haya? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tarimo, Mbunge wa Manispaa ya Moshi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeanzisha Mifuko kadhaa ambayo inawanufaisha Watanzania kulingana na eneo lile ambalo Mfuko huo umeanzishwa. Tunatambua kwamba kundi la vijana limechanganya maeneo yote, lengo pale ilikuwa ni vijana. Hata hivyo, iko Mifuko ya wananchi wote ambao pia wananufaika na Mifuko hii, lakini pia tumejiunganisha na taasisi za kifedha ambazo yeyote yule anakuwa na fursa ya kwenda kukopa.

Mheshimiwa Spika, tuliposema vijana, wanawake, wenye mahitaji maalum, Mheshimiwa Tarimo anajua kwamba sera ya nchi yetu sasa tumeelekeza katika kumwezesha mtoto wa kike, lakini na wanawake wote kwa ujumla ili na wao waweze kuchangia pato la nchi hii kwa kufanya shughuli mbalimbali. Kwa hiyo akishapata mkopo anaweza kuanzisha biashara na Mheshimiwa Tarimo anajua, ukimwezesha mwanamke unakuwa umeliinua Taifa hili. Ukimwelimisha mwanamke unakuwa umelielimisha Taifa hili. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tuliona eneo hili, kwa kuwa tunatambua kwamba ukimwezesha mwanamke unaliwezesha Taifa hili, ukimwelimisha mwanamke unaelimisha Taifa, kwa hiyo tuliona tuwawekee eneo lao ambalo wanakuwa na uhuru mkubwa wa kukopa. Anaweza kwenda kwenye Mfuko wa Halmashauri ambao una kipengele cha wanawake, anaweza kwenda Benki akakopa, anaweza kwenda kwenye Mfuko mwingine, Mifuko iko mingi, tuna Mifuko 42 ingawa sasa tutaipunguza ibaki michache, ifahamike kila mmoja aweze kwenda kukopa.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme tu bado hatujafikiria kuanzisha Mfuko wa Wanaume, lakini tayari wigo wa wanaume hao kupata mikopo upo kupitia Mifuko hiyo na taasisi za fedha. Hapo baadaye tukiona kuna umuhimu mkubwa, ama kuna udhaifu mkubwa pia tunaweza tukaanzisha kadiri itakavyowezekana. Sheria hizi na Mifuko hii tunapoianzisha tunaileta kwenye Kamati zetu za Bunge na kuona umuhimu wa kuanzisha hicho kitu. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister