Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2021-11-11

Name

Dr. Stephen Lemomo Kiruswa Mamasita

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Longido

Primary Question

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi niweze kumwuliza Waziri Mkuu swali. Kwa kuwa lengo la Sera ya Manejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma, ilitengenezwa toleo la pili mwaka 2008 ili kuboresha utumishi wa Umma na huduma zinazotolewa na Serikali kupitia watendaji wake kwa kuzingatia sifa na usimamizi unaotoa mwelekeo: Je, Mheshimiwa Waziri Mkuu…

SPIKA: Mheshimiwa naona kuna karatasi hapo mbele, kama vile unasoma. Hebu mwangalie Waziri Mkuu, halafu uliza swali.

MHE. DKT. STEVEN L. KIRUSWA: Mheshimiwa Waziri Mkuu, nilikuwa nataka kunukuu lengo la Sera ya Menejimenti na Ajira katika Utumishi wa Umma ambao unasisitiza kwamba watumishi wanaoajiriwa ni wale wenye sifa na ndio watakaosimamia matokeo tunayohitaji katika utendaji wa Serikali.

Na kwa kuwa tuna watumishi wengi wenye sifa katika ngazi ya kada za Watendaji wa Vijiji ambao wamefanya kazi hiyo kwa kujitolea kwa miaka mingi na kumekuwa na tatizo la kutoa vibali vya kuajiri:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuwaajiri ili kuondoa hiyo kero ya hawa watumishi ambao hawana ufanisi kwa sababu ni…

SPIKA: Ahsante sana. Umeeleweka Mheshimiwa.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kiruswa, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli tulianzisha mfumo ambao unaweza kuwafikia Watanzania wote katika kuajiri badala ya kuziachia sekta ambazo zilikuwa zinaajiri au kwa upendeleo au kwa namna ambayo wengi walikuwa wanalalamikia. Kwa kuunda Tume ya Ajira, tunakusanya nafasi kwenye taasisi zote zinazoombwa, tunaziombea kibali kwenye mamlaka. Tukishatoa kibali, Tume yetu inatoa tangazo Watanzania wanapata nafasi ya kuomba na kuitwa kwa ajili ya usaili halafu wanaweza sasa kuajiriwa.

Mheshimiwa Spika, hawa ambao wanafanya kazi kwa kujitolea kwenye maeneo yetu ya vijiji, kata na pia kwenye Halmashauri zetu wapo kwenye sekta kama afya na elimu, tunao. Wale wote ambao wanafanya kazi kwa weledi na wana sifa ya kuajiriwa, pindi tunapopata vibali kutoka Utumishi, tunawaajiri. Sasa hivi tumeshatoa maelekezo kwenye Halmashauri, wako vijana ambao wanafanya kazi kwenye Halmashauri zetu kwenye nafasi mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, kwenye sekta ya elimu wako walimu wanajitolea na wana nafasi nzuri; kwenye kata, pale kwenye mapengo tunao vijana kwenye vijiji vile, wanafanya kazi yao vizuri. Hawa wote tunaendelea kuwaangalia na kukusanya taarifa zao na sifa zao. Inapotokea kuwa na vibali ambapo sasa vinaendelea kuzalishwa kuajiri kada mbalimbali, itakapofikia kwenye kada hiyo, nao pia tunawapa nafasi ya kuwaajiri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali inaendelea kuwaangalia hawa wote ambao wamejitoa, wameamua kufanya kazi bila mshahara, lakini pia wanataka kuonesha uwezo wao na kuutumia muda wao vizuri kulisaidia na kulihudumia Taifa hili, wote wanapata kipaumbele kwenye ajira.

Mheshimiwa Spika, niwahakikishie wale wote ambao wanajitolea, tulikuwa tunazungumza na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, Mheshimiwa Ummy Mwalimu, juu ya vijana wetu ambao wanafanya kazi kwa kujitolea kule kwamba, hawa sasa waorodheshwe tuwatambue ili baadaye ajira inapotokea, waweze pia kuingia kwenye orodha ya waajiriwa. Kwa hiyo, huo ndiyo utaratibu ambao tunautumia kwa sasa. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister