Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2021-11-11

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, nashukuru sana nami kupata nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, magonjwa yasiyoambukiza; cancer, moyo na figo, yamekuwa yakitesa sana wananchi na yana gharama kubwa sana: Je, ni lini Serikali itaamua kuleta ile Bima ya Afya kwa wote ili kupunguza maumivu makubwa ambayo yanawapata kwa sababu gharama ni kubwa sana? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda, Mbunge wa Mkoa wa Mbeya, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba magonjwa haya sasa hivi nchini yamekuwa yanasumbua sana; cancer, magonjwa ya moyo, figo, pia hata BP, kisukari, ni miongoni mwa magonjwa ambayo Serikali kwa sasa imeyawekea msisitizo na mkazo kwamba yapewe kipaumbele katika kutoa tiba. Ndiyo maana kwenye sera yetu magonjwa haya kwenye maeneo mengi yanatolewa bure ili mgonjwa anapopata tatizo hili aweze kutibiwa bila gharama zozote.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na mchakato wa kukamilisha kuanza kwa Bima ya Afya kwa Wote. Tayari hatua za awali mpaka Baraza la Mawaziri imeshapitishwa; uko upungufu kidogo unatakiwa uimarishwe. Kwa sababu tunazungumzia Bima ya Afya kwa Wote, tunaendelea kupata uzoefu na ushauri na wadau kwa sababu Serikali ilianza na Bima ya Afya ile ya jamii inaitwa CHF; yako mafanikio na pia upo upungufu. Pia, tukawa na Bima ya Afya ya wafanyakazi NHIF ambayo pia nayo tumepata mafanikio, lakini pia changamoto zipo.

Mheshimiwa Spika, tunapokuja kuzungumzia Bima ya Afya kwa Wote sasa tunaanza kupata ule uzoefu tulioupata kwenye CHF na NHIF ili tuone namna ambavyo tutapanua na kumfikia kila Mtanzania, kila mmoja kwa pembe zote nchini ili tunapoanza Bima ya Afya tusiwe na upungufu mwingi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ndiyo hatua ambayo Wizara ya Afya inaendelea nayo kwa kushirikiana wadau, wale ambao wanatoa Bima ya Afya kwenye taasisi mbalimbali nao; hizi taasisi za bima ya kawaida ambapo pia nao wanatoa huduma ya matibabu ili tuweze kuweka utaratibu ambao utatufikisha. Kwa hiyo, Serikali sasa ikishakamilisha magonjwa hay ana wenzetu ambao wanapata tatizo hili tutakuwa kwenye nafasi nzuri ya kuhudumiwa. Kwa hiyo, nawaomba sana Watanzania mtuvumilie.

Mheshimiwa Spika, pia, Bunge letu tunaliomba lituvumilie, tukamilishe eneo hili ili tutakapokuwa tunaleta Bungeni tayari kwa kuanza, tuanze tukiwa tuna uhakika kwamba hatutakuwa na upungufu mwingi. Hiyo, ndiyo dhamira ya Serikali na tukishakamilisha hilo Muswada ule utaletwa hapa, utapitiwa na Waheshimiwa Wabunge ili tupate sasa mawazo yenu, mchango wenu na maoni yenu ya mwisho halafu tuidhinishe sasa Bima ya Afya kwa Wote iweze kuanza. Huo ndio utaratibu wa Serikali.

Additional Question(s) to Prime Minister