Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2021-09-09

Name

Flatei Gregory Massay

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mbulu Vijijini

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kunipa nafasi ya kuuliza swali kwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pamekuwa na wizi wa ng’ombe uliokithiri katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Mfugaji mara nyingi anapopata tatizo lolote anatumia ng’ombe wake kumsaidia na hao ng’ombe wamekuwa wakitolewa mkoa mmoja hadi mwingine pamoja na kuwa na chapa hizi alizozijibu katika swali la mwanzo.

Je, Serikali ina kauli gani kuhusiana na wizi huu?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Flatei Massay, Mbunge wa Mbulu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua hatua zinazochukuliwa na Serikali katika kudhibiti wizi wa mifugo.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge na Watanzania wote kwamba vyombo vyetu vya ulinzi nchini vimeendelea kufanya kazi kubwa sana na nzuri ya kudhibiti matukio ya uhalifu kote nchini ikiwemo la wizi wa mifugo na matukio mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye eneo la mifugo tunaendelea na udhibiti huo na tumetafuta njia rahisi ya kuweza kupunguza matukio haya. Moja, ni ile njia ambayo nimeijibu muda mfupi uliopita ya kuweka alama mifugo hii ili iweze kutambulika ni ya nani, ya eneo gani ili pale inapopotea tunaweza kuipata. Pia, tumeendelea kushirikisha wananchi kwenye ulinzi shirikishi kwa matukio yote ikiwemo wizi wa mifugo na wa namna nyingine yoyote ya uhalifu.

Mheshimiwa Naibu Spika, hatujaishia hapo, tumeendelea pia kushirikiana na wafugaji hawa kuhakikisha kwamba tunaweza kuimarisha ujenzi wa maeneo wanayoishi mifugo hii kwa mfano maboma yao, tumekuta maeneo mengine maboma yao wanazungusha tu miiba peke yake lakini ni rahisi ng’ombe hata kuruka na kuondoka na baadaye tunasema wameibiwa lakini kumbe boma lile siyo imara sana. Kwa hiyo, tumeendelea kutoa elimu ya uimarishaji wa maeneo hayo wanayohifadhiwa ng’ombe ili kuzuia wizi na wakati mwingine ng’ombe wenyewe kutoroka.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, tumedhibiti sana vibali vya usafirishaji holela kutoka eneo moja mpaka eneo lingine. Kama mwizi anaiba ng’ombe eneo A anawapeleka eneo B bila ya ukaguzi inakuwa ni rahisi sana sasa tulichofanya ni kudhibiti usafirishaji wa ng’ombe kutoka eneo moja mpaka lingine. Sasa ng’ombe hawezi kuhama kutoka kijiji kimoja mpaka kingine bila ya kibali maalum kinachotambulisha mwenye mifugo na kule anakokwenda. Hii ndiyo ambayo inasimamiwa sana kwa sasa ili kuweza kupunguza wizi wa mifugo kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea kutoa elimu kwa wafugaji lakini tunaendelea pia kufanya mikutano ya wafugaji kama nilivyosema ili haya mengine yote yanayojitokeza katika udhibiti wa wizi wa mifugo yaweze kupungua kwa kiasi kikubwa huku vyombo vya ulinzi vikiendelea na kazi yake ya ulinzi. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister