Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 53 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2021-06-17

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, Ilani ya Chama chetu cha Mapinduzi iliielekeza Serikali kuhakikisha kwamba usambazaji umeme vijijini unakamilika kufika mwaka 1922. Na Mheshimiwa Waziri Mkuu hivi karibuni kupitia Bunge hili Waziri mwenye dhamana ya nishati amekuwa akitueleza kwamba jukumu hili litakwenda kukamilika 2022 lakini pia ametupa mpaka namba za wakandarasi ili tufuatilie mwendelezo wa usambazaji umeme vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninayo masikitiko makubwa kwamba pamoja na agizo hilo, lakini sio vijiji vyote ambavyo vimeingizwa katika mpango huu; hivi tunavyozungumza wakandarasi wapo site lakini wanaruka baadhi ya vijiji kwa maana kwamba hawajapewa scope. Na zaidi ya hilo, badala ya nguzo 40 ambazo zilikuwa zinatolewa kwenye kila Kijiji sasa wanatoa nguzo 20. Sasa nilitaka kufahamu ni ipi kauli ya Serikali kuhakikisha kwamba ifikapo mwaka 2022 nchi nzima itakuwa inawaka umeme? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli Serikali imeazimia kupeleka umeme kwenye vijiji vyote na bado tumeweka dhamira ya kupeleka umeme mpaka vitongojini ikiwemo na maeneo ya visiwani. Utaratibu ambao tumeuweka ndani ya Serikali kwa zoezi hilo la kusambaza umeme, tunaenda kwa awamu na sasa tupo kwenye awamu ya tatu na hii awamu ya tatu tumeigawa kwenye awamu mbili; awamu ya tatu moja na awamu ya tatu mbili. Awamu ya tatu mbili imeanza siku za karibuni na wakandarasi tumeshawasambaza kwenye halmashauri zote ili kukamilisha vijiji vyote vilivyobaki vipate umeme. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kwenye awamu ya tatu hii mbili tumeongeza mkakati ambao nimeueleza awali wa kupeleka umeme kwenye vitongoji na kwenye visiwa kama vile kule Ukerewe, Mafia na maeneo mengine ya visiwa. Mkakati huu tayari umeshatangazwa, zabuni zimetolewa, wakandarasi wamepatikana, ujenzi wa umeme utaanza kazi mara moja. Lengo letu ni kupeleka umeme kila Kijiji na kupeleka umeme kwenye vitongoji vyote ikiwemo na visiwani ambapo tunaweza tukapeleka umeme jua ili nao wapate pia umeme kwa ajili ya matumizi ya kila siku. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, dhamira ya Serikali bado imebaki palepale na nakumbuka mwezi wa pili nilikuwa Mlalo kwa Mheshimiwa Shangazi kwa hiyo inawezekana ameuliza swali hili kama alivyokuwa amechangia siku ile kwenye mkutano wa hadhara na nikamhakikishia kwamba Serikali itapeleka umeme kwenye Jimbo la Mlalo lote, vijijini mpaka vitongojini. hivyo ni pamoja na nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote kwamba mkakati wa Serikali wa kupeleka umeme vijijini uko imara na sasa hivi tume-cover sehemu kubwa sana; tumebaki na vijiji vichache sana ili tuweze kuvimaliza vijiji vyote, kazi inaendelea na kwa kweli kazi inaendelea. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister