Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 43 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2021-06-03

Name

Ritta Enespher Kabati

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. RITTA E. KABATI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Serikali hii ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Rais wetu Samia Suluhu imeendelea kutoa matumaini makubwa kabisa kwa wawekezaji kuja kuwekeza hapa nchini. Hivi karibuni tumeona mfanyabiashara mkubwa kama Dangote amejenga imani na kuahidi kuwekeza zaidi hapa nchini lakini kumekuwa na changamoto nyingi sana katika kuwekeza hapa nchini. Je, nini mkakati wa Serikali kuhakikisha sasa hivi inatengeneza sheria bora na kujenga mazingira mazuri kwa ajili ya kuvutia wawekezaji kuja kuwekeza zaidi hapa nchini kwetu? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kabati, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ameomba kujua mkakati wa Serikali na maboresho yake kwenye uwekezaji. Watanzania wote mtakiri kwamba Serikali yetu imeweka msisitizo wa kuhakikisha kwamba tunapanua wigo unaowawezesha wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi kuja kuwekeza nchini kwa sababu fursa, malighafi na labor tunazo za kutosha. Sisi tunavutia uwekezaji kwa sababu maeneo mengi ya uwekezaji pia yanapunguza changamoto yetu ya ajira kwa Watanzania. Kwa hiyo, mfanyabiashara Dangote aliyekuja ambaye amewekeza kwenye kiwanda cha saruji Mkoani Mtwara ni miongoni mwa wawekezaji wakubwa nchini ambao pia tumetoa fursa za kupanua wigo wa uwekezaji wake.

Mheshimiwa Spika, nini Serikali inafanya kupanua wigo wa uwekezaji? Kwanza tunafanya maboresho ya sheria na kanuni zetu kwenye uwekezaji ili kujenga mazingira mazuri wezeshi ya uwekezaji nchini ili kila mwekezaji anayekuja kuwekeza apate huduma hiyo kwa ukaribu. Tumeanzisha taasisi inaitwa Tanzania Investment Center ambapo mwekezaji atapata huduma zote kupitia taasisi hiyo tunaita One Stop Center na tunaweza kumpa ardhi na aina yoyote ya msaada ambao anauhitaji katika uwekezaji wake. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Tanzania ya leo hatuna shida ya ardhi, ardhi tunayo, umeme upo wa kutosha, maji tunayo, barabara zetu nzuri na mazingira ya uwekezaji Tanzania sasa ni mazuri. Sheria hizi ambazo tunaendelea kuzirekebisha na kuzifanya kuwa sheria wekezi zitasaidia sana wawekezaji kuja nchini kama ambavyo tunaona sasa kasi ya wawekezaji kuja kwenye maeneo haya imeongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge na wawekezaji wote mliopo ndani ya nchi na walio nje ya nchi kuja Tanzania kuwekeza kwa sababu mazingira ya uwekezaji yanaendelea kuboreshwa. Sasa hivi tunakaribia kuweka ile sheria ambayo imekusanya changamoto nyingi ambazo zilikuwa zinawakwaza wawekezaji na mengine ni ya kisheria kwa hiyo tunafanya maboresho ya sheria ili kuondoa vikwazo vya uwekezaji Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia tunataka tuainishe huduma ambazo sisi tunazitoa au fursa zilizopo Tanzania ili kuhakikisha kwamba tunafanya wawekezaji kuwa na imani nasi. Wiki iliyopita nilikuwa Mkoani Mara kwenye mkakati wa kutangaza vivutio vya uwekezaji. Huu ni mwendelezo wa kutangaza fursa za mikoa yote nchini ambapo mpaka sasa tumeshafika mikoa 24 kuhakikisha kwamba tunawaonesha wawekezaji nini kipo kwenye mkoa huo ili kila mmoja aamue kwenda mahali anapotaka. Tuna malighafi nyingi sana zinazogusa kwenye sekta ya kilimo, madini na maliasili, hizi zote pia zinasaidia uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba tunaendelea kufanya maboresho haya mara kwa mara ya kupitia changamoto tulizonazo na tunaziingiza kwenye sheria ili tuwe na sheria endelevu ambayo pia inaweza kutusaidia kuwekeza. Yale yote ambayo yanajitokeza kwa sasa tunayachukua, tunayafanyia utaratibu wa kuyaboresha hivyo na kurahisisha uwekezaji huo kwa yeyote anayetaka kuwekeza hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, hata hili suala la vibali vya kazi tumeendelea kufanya maboresho ili wawekezaji sasa wawe na uhakika wa kuleta watu wao kuja kuwekeza hapa na mambo mengi ya uwekezaji ambayo yapo kwenye kile kitabu kinaitwa Blue Print ambacho kina maelekezo yote ya uwekezaji. Niendelee kuwahakikishia Watanzania fursa tulizonazo zitatusaidia pia sana kunufaisha Taifa letu.

Kwanza mwekezaji akija tutapata kodi lakini mbili ushiriki wa Watanzania, tatu ajira lakini nne malighafi na mazao tunayoyalima pia yanapata soko. Kwa hiyo, jambo hili kwa ujumla wake lina faida kubwa na sisi tunalisimamia kuwa linaleta tija kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba kulijibu kwa upana huo ili wawekezaji wote wanaotaka kuja nchini waje kuwekeza na sisi tunawakaribisha. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister