Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 43 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2021-06-03

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, zao la chai lina soko kubwa sana hapa nchini na hata soko la dunia. Nini kauli ya Serikali juu ya wakulima wa chai wanaolima chai lakini chai hiyo inauzwa kwa bei ya chini sana na kuwanufaisha watu wa katikati ambao wao hawawezi kusaidia hawa wakulima wakaweza kukidhi mahitaji yao?

Naomba kauli ya Serikali juu ya bei ya chai hapa nchini Tanzania. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda, Mbunge, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, mazao yetu haya chai ikiwemo Serikali inaendelea kuyasimamia kuanzia kilimo mpaka masoko yake na malengo ya Serikali ni kumnufaisha mkulima aweze kupata tija ya kutosha kwa kuuza bei nzuri kwenye masoko yetu.

Nakiri kwamba tunayo changamoto kwenye masoko ya zao la chai, hata tulipokuwa kwenye kikao pale Njombe miezi miwili iliyopita tulizungumza kwa kina juu ya tatizo la soko la zao la chai ambalo kwa sasa minada yake inategemewa sana kufanywa nchini Kenya kwenye Jiji la Nairobi pekee badala ya minada ile kuendeshwa hapa nchini na kuongeza gharama za uendeshaji wa zao hili kuliko kama tungeweza kuanzisha mnada hapa. Makubaliano ambayo tumefanya pamoja na wadau ni kuanzisha soko hapahapa ndani ya nchi ili kuwezesha zao hili kupata bei nzuri kwenye masoko yetu na kuwataka wanunuzi waje nchini wanunue hapa na kwa hiyo itapunguza gharama za uendeshaji wa mkulima mwenyewe na wengi wapo kwenye ushirika na ushirika wenyewe ili bei ile iweze kumsaidia mkulima kuweza kulilima tena zao hili na kulifanya kuwa endelevu.

Mheshimiwa Spika, katika miaka/mitatu iliyopita tumepata changamoto sana, nimetembelea Rungwe kwa Mheshimiwa Mwakagenda, nimetembelea kwenye kiwanda lakini nimezungumza na wakulima pale Rungwe nimeona tatizo kubwa miaka hii miwili/mitatu unaotokana na ugonjwa wa Covid kwamba masoko yetu kule tumeshindwa kuyafikia na kwa namna hiyo hata wanunuzi wamekuwa hawaamini kununua mazao kwa umbali pamoja na kwamba tuna mifumo ya kielekroniki, hata hivyo bei zake zimekuwa za chini sana. Kwa hiyo, tunachofanya hapa, tunaendelea kupunguza hao watu wa kati ambao wanazidi kupunguza faida ya mkulima na kumfanya mkulima moja kwa moja kupitia ushirika wake aingie kwenye mnada ambao tumeupanga kuufanya humuhumu ndani. Hivyo ndiyo njia sahihi ambayo tunadhani inaweza kutusaidia pia kumfanya mkulima apate fedha yake moja kwa moja badala ya watu wa kati ambao wakati mwingine wanafanya thamani ya zao kupungua.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Serikali tunaendelea kuona na kubaini masoko kupitia Balozi zetu kuona ni Balozi ipi nchi hiyo inahitaji chai ili tufanye mauzo ya moja kwa moja na nchi hiyo ili zao letu kwa kweli liweze kupata bei. Kwa hiyo, jitihada za Serikali zinaendelea na niwahakikishie Watanzania kwenye mazao yote chai ikiwemo, tunaendelea kujitahidi kuhakikisha kwamba tunapata masoko ya uhakika ili wakulima wetu wote wapate faida kwenye kilimo wanachokilima na hasa kwa kutafuta mifumo mizuri ya masoko. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister