Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 43 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2021-06-03

Name

Iddi Kassim Iddi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Primary Question

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante. Tunatambua kwamba Serikali yetu ilizuia kabisa usafirishwaji wa makinikia nje ya nchi na kwa sasa tumeshuhudia makontena ya makinikia yakisafirishwa kupitia barabara ya Bulyanhulu – Kahama na Bandari yetu ya Dar es salaam hivyo kupelekea taharuki kwa Watanzania na kwa wananchi wa Jimbo la Msalala. Nini sasa kauli ya Serikali juu ya jambo hili? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nami nimeona pia kwenye mitandao watu wakionesha kwamba wanaona makontena ya makinikia yakisafirishwa kwenda nje. Nataka niwakumbushe Watanzania kwenye hili kwamba mwaka 2017/2018 tulizuia usafirishaji wa makinikia kwenda nje ya nchi kwa sababu yalikuwa hayajafuata utaratibu lakini pia kulikuwa na udanganyifu mkubwa. Tulipozuia makontena zaidi ya 300/400 yaliyokuwa bandarini yalikaa pale mpaka tulipoweka utaratibu. Utaratibu uliowekwa na Serikali kwanza kuwatambua ni nani wanasafirisha makinikia kwenda nje na ni nani wametoa vibali hivyo kwenda nje na tukazuia kabisa tukaanza utaratibu mpya.

Mheshimiwa Spika, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wa Awamu ya Tano alilisimamia na kwa kuunda timu iliyofanya uhakiki wa sekta yote ya madini ikiwemo na eneo hili la usafirishaji mchanga ambalo kwa kweli tulikuwa tunaibiwa kwa kiasi kikubwa. Ufumbuzi wa ile timu ni kuanzisha kampuni ya Watanzania kwa ushirikiano na makampuni ya nje yaliyopo hapa nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, leo hii tunayo kampuni inaitwa Twiga Minerals ambayo ni ya Watanzania kwa maana ya Serikali ambayo imeingia ubia na hao wachimbaji wakubwa wa madini kwenye mgodi kama ule wa kwako Mheshimiwa Mbunge wa Bulyanhulu lakini wa pale Kahama Mjini Buzwagi na kule Tarime North Mara. Migodi hii mitatu chini ya Barrick tumetengeneza kampuni ya pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwanza wataalam baada ya kuchimba tunapitia kujua aina zote za madini. Mwanzo tuliambiwa madini yaliyopo pale ni ya aina moja tu dhahabu lakini kumbe kule ndani baada ya ukaguzi na uchunguzi wa wataalam tumegundua tuna aina tano za madini. Kwa hiyo, leo hii kupitia Kampuni yetu ya Serikali, inauza madini ya aina zote 5 siyo moja kama zamani. Mbili; tukishapata ule udongo na ukaguzi huo na kugundua aina zote, tunayauza hapahapa ndani ya nchi, sio nje ya nchi. Makontena yote yanayosafirishwa tayari yameshauzwa, Serikali imeshapata fedha yake na fedha imeshahifadhiwa kwenye akaunti zetu kwa hiyo Watanzania hatupati hasara. Hatua inayofuata mnunuzi anakuwa huru kuyapeleka anakotaka na ndio hayo ambayo yanaonekana kutoka. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Watanzania kuyaona makontena yakipita na hofu ya awali, nataka niwaondolee kuwa makontena hayo yameshauzwa tayari na huyo ni mnunuzi. Kwa hiyo, waondoe mashaka juu ya usafirishaji wa makontena hayo yenye makinikia kwa sababu Serikali iko makini sana. Inayo timu palepale kwenye mgodi ya kuhakiki lakini pia ya mauzo na kuhakikisha fedha inalipwa na hakuna kontena linatoka nchini bila kuuzwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tumeweka timu pale bandarini kuhakikisha kwamba kila kontena la makinikia linaloingia pale lina nyaraka zote baada ya kufanya mauzo hukohuko kwenye mgodi, kwa hiyo, hakuna kontena linaibiwa. Kwa hiyo, Watanzania muondoe mashaka, Serikali ipo makini, watu wetu tuliowaweka kwenye maeneo haya kuhakiki kuwepo kwa nyaraka zote za kuuza makinikia hayo zipo makini na kwa kweli tunaingiza fedha za kutosha; sina takwimu za kutosha lakini tuna fedha ya kutosha kwa sasa. Mheshimiwa Waziri wa Madini alipokuwa anawasilisha bajeti yake hapa alitoa ufafanuzi na kuonesha namna ambavyo kwenye madini tumepata fedha kiasi kikubwa sana. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister