Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 43 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2021-06-03

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kwanza kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, swali langu litahusu sekta ya korosho. Mwaka huu tumepata taarifa kwamba Serikali ilijipanga kutupatia pembejeo wakulima wa zao la korosho kwa maana kwamba waje kuzilipa baadaye kwenye mjengeko wa bei. Hata hivyo, kuna taharuki kubwa kwa wakulima wetu wa korosho baada ya Bodi ya Korosho kuleta waraka kwenye Halmashauri zetu, wakiwaambia kila mkulima akipeleka zao lile kwenye mnada kila kilo moja itakatwa shilingi 110 bila kujali kwamba mkulima yule amechukua pembejeo kwa kiwango gani. Barua ile inasema kwamba jambo hili hata sisi Wabunge tumeliridhia.

Mheshimiwa Spika, sasa kuna taharuki kubwa sana kiasi kwamba mpaka…

SPIKA: Swali lako ni nini katika jambo hilo?

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, kutokana na mkanganyiko huu ni nini kauli ya Serikali ili wakulima wetu waendelee kuchukua zile pembejeo maana sasa hivi wanaziogopa.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Wizara yetu ya Kilimo imetoa miongozo kadhaa ya kuboresha masoko ya mazao nchini ili kuwanufaisha wakulima kwenye mazao wanayoyalima ikiwemo na kuwarahisishia namna nzuri ya kupata pembejeo. Zao la korosho ni miongoni mwa mazao ambayo Serikali kupitia Wizara ya Kilimo imeendelea kufanya mapitio ya maboresho ya namna nzuri ambayo wakulima ambao kwa sasa ndiyo wapo kwenye msimu wa kutumia pembejeo ili waweze kupata pembejeo wakulima wote na waweze kushiriki vizuri kwenye kilimo hiki.

Mheshimiwa Spika, nakiri kwamba ipo taharuki kwa sababu na mimi ni mdau pia wa zao hilo lakini taharuki hii imetokana na vikao vya awali vya majadiliano ya mfumo mzuri ambao pia wakulima nao wanaweza kushiriki vizuri kupata pembejeo. Si kwamba Wabunge wameshiriki katika kutoa maamuzi, hapana, bali Wizara inaendelea kuwa na vikao vya mara kwa mara ili kufikia hatua nzuri ya kuwezesha kila mkulima kupata pembejeo. Vikao hivi bado havijakamilika na kikao kikubwa kabisa kipo tarehe 6 ambacho kinaalika wakulima, viongozi wa ushirika, viongozi wa Serikali na Waheshimiwa Wabunge pia mtaalikwa ambacho sasa tutajadili namna nzuri ya kumwezesha mkulima kupata pembejeo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, maelekezo ya awali ya kwamba kila mkulima atakatwa shilingi 110 yamesitishwa kwa muda ila wakulima wote waende kupata pembejeo zile ambazo zimepelekwa kwenye maeneo yale. Kiwango cha pembejeo kilichoagizwa kinatosha kabisa kwa kila mkulima kutokana na takwimu zilizopatikana kutoka vyama vyetu vya ushirika ili kila mkulima apate pembejeo ya kutosha kupuliza awamu zote nne kufikia kipindi cha uzalishaji. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kikao kile cha tarehe 6 ndicho kitakachotoa mwelekeo mzuri wa nini kitafanyika kwa pembejeo ambazo zimetolewa na wala haitakuwa kumkata kila mkulima kwa kilo aliyoipeleka sokoni kwa sababu wapo wengine wana kilo mbili, wengine kilo 10 lakini wapo wamezalisha zaidi ya tani 20, sasa huwezi kukata kwa kila kilo. Kwa hiyo, hilo linafanyiwa kazi na Wizara na ufafanuzi utatolewa siku ya tarehe 6 ambapo wadau wa zao la korosho kila mmoja atashiriki kwenye eneo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwasihi wakulima wa zao la korosho waendelee kupokea pembejeo zile. Serikali inaendelea kuangalia namna bora ya kumfanya mkulima aweze kupata pembejeo kwa gharama nafuu ili aweze kuendelea kulima zao hilo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niongezee eneo lingine ambalo pia limeleta mkanganyiko kwamba mabenki ambayo miaka yote yamekuwa yakitoa mikopo kwa wakulima, mwaka huu walisimama kutoa mikopo yao kwa hofu kwamba wakulima watakapopata pembejeo huku Serikalini hawataweza kulipa gharama ya mikopo ambayo wameikopa kwenye mabenki. Tumeruhusu mabenki yaendelee kukopesha wakulima kwa sababu bado kwenye zao la korosho kuna shughuli nyingi za kufanya; pamoja na kupilizia dawa lakini pia kuna kupalilia, kuokota na kuhakikisha zao linakwenda sokoni, yote inahitaji mtaji ambapo mkulima ambaye amelima, anajiamini kwamba atakopa na kurejesha, bado mabenki yaendelee kukopesha. Tumeshawapa maelezo hayo mabenki na wanaendelea na kukopesha. Kwa hiyo, wakulima waende wakakope kulingana na mahitaji yake ili alihudumie zao na hatimaye aweze kurejesha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, napenda kuwaambia Waheshimiwa Wabunge wote wanaotoka kwenye majimbo yanayolima zao la korosho muendelee kuiamini Serikali na mifumo ambayo inaendelea kuipanga. Mifumo hii haiamuliwi tu moja kwa moja na Serikali bali inashirikisha wadau na kwa zao la korosho wadau tutakutana siku ya tarehe 6. Kwa hiyo, siku hiyo tutatoa mwelekeo wa zao hilo sote kwa Pamoja. Kwa hiyo, wawe na amani na waendelee na uratibu wa zao hili la korosho, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister